Tuesday, June 12, 2012
Y A M U Y A M U P E D E J H E E !
NGOJA niwasimulie, mengi msiyoyajua,
Ili kesho msilie, eti hamkuambiwa,
Dunia usiitanie, ni shushu umeumbiwa,
Yamuyamu pedejhee, nyamunyamu moto pia !
Dunia usiidhanie, ni rafiki wa kufaa,
Ni pai umgundue, mambo atahadithia,
Kizimbani uingie, ushahidi akatoa,
Yamuyamu pedejhee, nyamunyamu moto pia !
Sikia niwaambie, kitu hatosingizia,
Ila yote ayatoe, ukweli tupu ukawa,
Pakwenda usipajue, ukabaki unalia,
Yamuyamu pedejhee, nyamunyamu moto pia !
Tamu tamu pedejhee, puani utakitoa,
Motoni uungulie, moto mali yako kuwa,
Haya yangu uchungue, dhihaka kutofanzia,
Yamuyamu pedejhee, nyamunyamu moto pia !
Usiache 'kunogee, pepo ukaidhania,
Ni matete yatetee, kiziwi kutosikia,
Ni tambaa liondoe, upofu kutoingia,
Yamuyamu pedejhee, nyamunyamu moto pia !
Na mja ujitambue, kwanini umezaliwa,
Haukuja ufukiwe, chochote kutojaliwa,
Machoni uondolewe, utupu ukabakia,
Yamuyamu pedejhee, nyamunyamu moto pia !
Anisi uzingatie, kiumbe kujitambua,
Vingine huja isiwe, uishi umeishiwa,
Na kitanzi ujitie, taabu kutovumilia,
Yamuyamu pedejhee, nyamunyamu moto pia !
NI hadithi muijue, adili iliyojaa,
Na wajinga wazingue, simulizi kukataa,
Mpaka yawafikie, wenzi wakasimuiia,
Yamuyamu pedejhee, nyamunyamu moto pia !
Ibakie hatimaye, na laiti ningejua,
Kikaingia kiwewe, dhiki unaowaachia,
Wabondwe wasibandue, viraka vya kufulia,
Yamuyamu pedejhee, nyamunyamu moto pia !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment