Thursday, June 14, 2012

Lipi wakusaidia ?



Wasiwasi waugua, kitako kutotulia,
Mwanangu nakwambia, ni bure yako fadhaa,
Huna unalougua, ila kisaikolojia,
Lipi wakusadia, wasiwasi wako bure !

Hayo ukiyakataa, uzima ukajitia,
Hutoipata fadhaa, na moyo utatulia,
Ila ukiendelea, pabaya utaingia,
Lipi wakusadia, wasiwasi wako bure !

Moyo fanza kuridhia, la Mola huja timia,
Hofu unapoitia, bure unajionea,
La kuwa budi likawa, lisokuwa, kutokuwa,
Lipi wakusadia, wasiwasi wako bure !

Bure unajisumbua, la kuwa budi likawa,
Hapana wa kuzuia, lazima litatimia,
Kadari ukiijua, Mola utamuachia,
Lipi wakusadia, wasiwasi wako bure !

Madogo kutokukuzua, makubwa ukaachia,
Jengo ulilojaliwa, wapaswa kuangalia,
Ni mwili uliopewa,  na Mola wetu Jalia,
Lipi wakusadia, wasiwasi wako bure !

Udokta aujua, hata hewa kuwa dawa,
Na dua ukizijua, balaa huliondoa,
Huko ukishazamia, hofu utaiondoa,
Lipi wakusadia, wasiwasi wako bure !

Umri nakuombea, nyuma ukanifatia,
Mazuri kuja kuzua, nchi ikajivunia,
Nawe budi kutulia, Mola ukamuachia,
Lipi wakusadia, wasiwasi wako bure !

No comments: