Monday, June 18, 2012

Watu ni sisi wenyewe



Chetu ni nani kavaa, kiatu tulichopewa,
Atakiwa kukivua, wenyewe tukakivaa,
Sivyo atatuchezea, na uhuni kutufanyia,
Watu ni sisi wenyewe, kiwapikiatu chetu ?

Katiba yatuambia, ndivyo ninavyotambua,
Madaraka tumepewa, na mamlaka kujaliwa,
Nchi kuisimamia, kwa umoja wetu tukiwa,
Watu ni sisi wenyewe, kiwapikiatu chetu ?

Kazi tunaowaachia, ukubwa si kuchukua,
Mabosi tunabakia, hili wapte kujua,
Uongo wakiutia, mara moja kuwatoa,
Watu ni sisi wenyewe, kiwapikiatu chetu ?

Uwizi tukisikia, hakuna kuwaachia,
Watu sasa wamejaa, kazi hizo wazijua,
Ofisi waking'ang'ania, ni budi kuwatimua,
Watu ni sisi wenyewe, kiwapikiatu chetu ?

Rushwa wakiipokea, au fisadi kuachia,
Pasiwe na kuchelewa, lazima kuwatimua,
Ubosi tuantakiwa, wao wapate tambua,
Watu ni sisi wenyewe, kiwapikiatu chetu ?

Katiba inatakiwa, mpya ikitujia,
Hili kulitambua, na mengine kuyazua,
Kinga ikaondolewa, maovu tukifichua,
Watu ni sisi wenyewe, kiwapikiatu chetu ?

Kuna vyombo wameua, sisi tunawaachia,
Twazidi kuvumilia, nchi inadidimia,
Haya yasingelikuwa, uwajibikaji ukiwa,
Watu ni sisi wenyewe, kiwapikiatu chetu ?

Kuna uongo  watia, hata wanapotambua,
Na ukweli kufukia, ili kufanza hadaa,
Hakika wanatakiwa, watu hawa kutokaa,
Watu ni sisi wenyewe, kiwapikiatu chetu ?

Hazina waidonoa, kwenda wao kuwafaa,
Katiba tukifatia, tungekwishaondoa,
Ila bado twapumbaa, mpya kuingojea,
Watu ni sisi wenyewe, kiwapikiatu chetu ?

Watu sasa kutmbua, uongozi sio raha,
Yaweza kugeukia, makini usipokuwa,
Ukubwa wenye balaa, watu wanaukataa,
Watu ni sisi wenyewe, kiwapikiatu chetu ?

No comments: