Thursday, June 14, 2012

Dhihaka n'ache kutoa



Nimekwishajichumia, kivulini ninakaa,
Na kila siku natia, vyote vinavyokolea,
Nani wa kumfikiria, bure nikajisumbua ?
Dhihaka n'ache  kutoa, tumbo langu linajaa ?

Mtaji nishajipatia, kwa mbovu Tanzania,
Na njia ninazijua, vitu nikajivutia,
Kwangu vikajipitia, kunawiri kwendelea,
Dhihaka n'ache  kutoa, tumbo langu linajaa ?

Tumbo langu linajaa, masikio yafuaa,
Siwezi kuwasikia, kilio mnacholia,
Sasa najitafunia, niwezeje kuongea ?
Dhihaka n'ache  kutoa, tumbo langu linajaa ?

Malipo narudishiwa, mikopo niliyotoa,
Na bure nilivyogawa, wala waliojaliwa,
Nami hivyo changu pia, niacheni kujilia,
Dhihaka n'ache  kutoa, tumbo langu linajaa ?

Huwezi ukawa dawa, kwa wote kwenye dunia,
Kundi limeshatimia, wengine nawaachia,
Ila nikishaambiwa, budi nitawaumbua,
Dhihaka n'ache  kutoa, tumbo langu linajaa ?

Dhihaka nitaitia, na mimi nikasifiwa,
Kusema sana najua, maana yasiyokuwa,
Ila kambi kutetea, wa taifa nilokuwa,
Dhihaka n'ache  kutoa, tumbo langu linajaa ?

Hata mkinichukia, nilikwishaandikiwa,
Yote yangu yatimia, katika hii dunia,
Hayo yakuyangojea, nyie ninawaachia,
Dhihaka n'ache  kutoa, tumbo langu linajaa ?

Urithi sijangojea, changu nimeishachukua,
Changu wasije kitwaa, ndo hivyo nawatetea,
Nchi inaendelea, ila vipofu mmekuwa,
Dhihaka n'ache  kutoa, tumbo langu linajaa ?

No comments: