Sunday, June 17, 2012

Tabia hii si njema


Haifai maamuma, na pia ina imamu,
Dhambi bure ukachuma, kwa yasiyo umuhimu,
Katika zenu kalima,na vitendo kuvikimu,
Tabia hii si njema, ya riha na kujiona.

Wapo wasiyo rahima, watu wanaodhulumu,
Kwa kujifanza adhama, na eti watu muhimu,
Dunia wakaihama, hali sio marhumu,
Tabia hii si njema, ya riha na kujiona.

Ya dini wakayakama, na kuyatia hukumu,
Akili zikawahama, zikatinga jehanamu,
Ya uongo kulalama, ya wengine yawe magumu,
Tabia hii si njema, ya riha na kujiona.

Kioo hujitazama,  wengine kuwahukumu,
Yawaishia hekima, imani kuzihasimu,
Na Mola ni muadhamaawajua  mahadhamu,
Tabia hii si njema, ya riha na kujiona.

Huichezea neeema, kufanza wengi hadimu,
Wakajitia karama, zimekwishawasalimu,
Na yao bila kusoma, yaweza kutakadamu,
Tabia hii si njema, ya riha na kujiona.

Hawaipata karamu, na wengine hudhulumu,
Akaitoa Karima, kwake walio rahimu,
Wakaifanza hujuma, kuhukumu binadamu,
Tabia hii si njema, ya riha na kujiona.

Ukubwa huuazamia, wakajifanza kaimu,
Nchi wakaisakama, ya kwao yapate dumu,
Wakazizua nakama, tena daima dawamu,
Tabia hii si njema, ya riha na kujiona.

Hakika hawajasoma, ya kheri wayashutumu,
Busara zinshawahama, na ualimu adimu,
Upofuni wanazama, nia yako kukirimu,
Tabia hii si njema, ya riha na kujiona.

Dunia itasimama, kwa wao kuihumu ?
Yake yeye wamehama, na sanaa waadhimu,
Kinawangoja kiama, kikawafanza karamu,
Tabia hii si njema, ya riha na kujiona.

Haitozama neema, kwa layli na kiamu,
Zitafutika hujuma, fitna za wanadamu,
Kwao ikawa gharama, na wenyewe madhulumu,
Tabia hii si njema, ya riha na kujiona.

Mioyo itaegema, kumtwii ya Karimu,
Na palipo na zahama, akaondoa ugumu,
Kwetu yakawa uzima, na kwao ni marhumu,
Tabia hii si njema, ya riha na kujiona.

Yatakuja kusimama, wao wasiyo azimu,
Muumini akasoma, na kuzijua hukumu,
Ikijaiika rehema, heri wakaisalimu,
Tabia hii si njema, ya riha na kujiona.

Waipatao heshima, wengine hawahukumu,
Na walio na hikma, wengine hawadhulumu,
Na mtu kuwa salama, ya watu asihujumu,
Tabia hii si njema, ya riha na kujiona.

Utukufu wa Alima, mkuu wa mahakimu,
Yake ndio husimama, sio wanaodhulumu,
Kiumbe aso rehma, yake huwa hayadumu,
Tabia hii si njema, ya riha na kujiona.

Waipatao heshima, wengine hawahukumu,
Na walio na hikma, wengine hawadhulumu,
Na mtu kuwa salama,ya watu asihujumu,
Tabia hii si njema, ya riha na kujiona.

Hizi ni nyingine zama, kafiri wanasilimu,
Mtu hapati heshima, kwa majoho na kalamu,
Kama anayoyasema,yanukia udhalimu,
Tabia hii si njema, ya riha na kujiona.

Waipatao heshima, wengine hawahukumu
Na walio na hikma, wengine hawadhulumu,
Na mtu kuwa salama,ya watu asihujumu,
Tabia hii si njema, ya riha na kujiona.

Au wanaojinoma, na kujifanza rahimu,
Hadaa wakazitema, na umbeye kukirimu,
Huzaa yao lawama, yalojaa Jahanamu,
Tabia hii si njema, ya riha na kujiona.

Waipatao heshima, wengine hawahukumu,
Na walio na hikma, wengine hawadhulumu,
Na mtu kuwa salama,ya watu asihujumu,
Tabia hii si njema, ya riha na kujiona.

Hapa ninatia tama, muda nisiwadhulumu,
Tuitafute rahma, kwa umoja kuukimu,
Wamoja tukisimama, yatakwisha madhulumu,
Tabia hii si njema, ya riha na kujiona.

No comments: