Thursday, June 14, 2012

Wabunge wa Tanzania


Shindano: Mchuano wa Kuzunngumza Kiingereza !


Wabunge wa Tanzania, lugha mnayoiua:
Kiswahili maridhia,  sisi tuliyejaliwa,
Leo kikawa kinyaa,  hakifai kutumiwa,
Shindano naliandaa, Kingereza kuongea !

Wabunge wa Tanzania, lugha mnayoiua:
Kuongea mtatakiwa, mada mnapozitoa,
Ung'eng'e tu kutumia, kuanza na kuishia,
Bila maneno kutia, Kingereza yasokuwa !


Wabunge wa Tanzania, lugha mnayoiua:
Kama ni li moja saa, au yakawa masaa,
Kiswahili kubabia, katu halitokubaliwa,
Ushindi hamtopewa, ila kulipa fidia !


Wabunge wa Tanzania, lugha mnayoiua:
Sasa nachangamkia, wafadhili kwa mamia,
Lugha wanaoililia, izidi kuendelea,
Ili wapate changia, fuko langu la  hidaya!


Wabunge wa Tanzania, lugha mnayoiua:
Kiasi nikikijua, fomu nitawatumia,
Mjaze kwa njema nia, shindanoni kuingia,
Kila fomu naambiwa, milioni itakuwa !


Wabunge wa Tanzania, lugha mnayoiua:
Zawadi zawangojea, majuu kwenda paa,
Mkamwone Malkia, na Buckingham kuingia,
Na siri mkagundua, huko miktembelea !


Wabunge wa Tanzania, lugha mnayoiua:
Na siri mkagundua, huko miktembelea,
Kuandika wasojua, Kiingereza waongea,
Kusoma wasiojua, Uingereza wamejaa!

Wabunge wa Tanzania, lugha mnayoiua:
Kasumba ikiwaishia, la kwenu mtalijua,
Aali kuazimia, nchi ipate endelea,
Mzaha nazo nazaa, ktu hazitosaidia !

No comments: