Tuesday, June 12, 2012

N I P E N D E N I K I W A H A I !


Nienzi nikiwa hai, ningali ninapumua,
Kuniafu jitimai, na langu kulisikia,
Na dua kunistahi, dhambi nikapunguziwa,
Nipende nikiwa hai, usinipende maiti !

Njoo unigee rai, na afua si mafua,
Sautiyo iwe nai, nikapata kusinzia,
Ni yanini baibai, na nyuma wanifatia ?
Nipende nikiwa hai, usinipende maiti !

Yako yawe ni anwai, wasipate kusikia,
Niletee na mayai, kienyeji yalokuwa,
Nikaangie na chai, pamoja na kitumbua,
Nipende nikiwa hai, usinipende maiti !

Nipende ukijiwahi, waona nakwangalia,
Na mcho hayatulii, kope  yafuatilia,
Kama unayo madai, usiache kumbushia,
Nipende nikiwa hai, usinipende maiti !

Nipende ninafurahi, moyo ukakuridhia,
Na kama ni asubuhi, karibu ukajongea,
Tupate staftahi, wawili tunaongea,
Nipende nikiwa hai, usinipende maiti !

Naugua, siugui, hali yangu kuijua,
Madhali ningali hai, tunawez kuongea,
Ujualo silijui, laweza likawa dawa,
Nipende nikiwa hai, usinipende maiti !

Naweza nikawa hoi, kukuona nikapoa,
Ana ibra Muhyi, huwezi kuziagua,
Ghaibu hazitulii, ukaribu zakataa,
Nipende nikiwa hai, usinipende maiti !

Nikiwa ni goigoi, waweza kunichapua,
Hilo haliwi jinai, si shida kulitambua,
Moyowe siuchukui, mwilini utabakia,
Nipende nikiwa hai, usinipende maiti !

Mimi sio Mmasai, maiti kuikimbia,
Ila sababu sijui, maiti kuchungulia,
Nifateni niko hai, mfu sintawasikia,
Nipende nikiwa hai, usinipende maiti !

Ila sababu sijui, maiti kuchungulia,
Yangu ninatoa rai, mapema kuifukia,
Islamu na jamii, nakataa kukawia,
Nipende nikiwa hai, usinipende maiti !

Wachamungu nawasihi, ombi langu kusikia,
Msitafute rai, tosha dua kuitia,
Na ubani pia udi, msiache nichomea,
Nipende nikiwa hai, usinipende maiti !


No comments: