Sunday, June 17, 2012

Nadra mafanikio


UONGO palipojaa, vigumu kufanikiwa,
Ni jangwa palipokuwa, kitu hakiwezi mea,
Hupakimbia mvuu, ukame ukazidia,
Vigumu kufanikiwa, palipojaa uongo !

Fisadi walipojaa, kuifasidi dunia,
Kila kiumbe hunywea, na mioyo ikavia,
Huruma ikapotea, pakabaki maasiya,
Mafanikio nadra, palipojaa fisadi !

Watu wakiwa bidhaa, rahisi kununuliwa,
Malaika hukimbia. pembeni kujikalia,
Mungu wakamlilia, haki yake kuitoa,
Vigumu kufanikiwa, watu wakinunuliwa !

Zikiingia sanaa, maisha kuyatania,
Uhai mara huvia, na mioyo kudumaa,
Pasiwe la kusikiwa, sembuse kufanikiwa ?
Mafanikio nadra, palipo na usanii !

Uonevu ukijaa, chozi dunia hutoa,
Ardhi 'kajinamia, watu kusikitikia,
Na mbingu kujipasua, kwa hasira kuijaa,
Vigumu kufanikiwa, uonevu ukijaa !

Dhuluma ikiingia, nchi huwa yatitia,
Na bahari kutanua, nchi ikaivamia,
Kilio kikasambaa, hata ng'ambo kufikia,
Vigumu kufanikiwa, dhuluma ikitawala !

Watu wanakozomea, bila kitu kuelewa,
Vitabu  hujifunua, orodha ikaitia,
Wajinga waliojaa, hadi nchi kulemaa,
Vigumu kufanikiwa, watu wanakozomea !

Roho zikiwa bandia, unafiki ukajaa,
Mazuri huwakimbia, yakabakia mabaya,
na uoza ukajaa, kushoto pia kulia,
Mafanikio nadra, kwa mapambo ya bandia !

Rushwa ikivumuliwa, kama halali ikawa,
Askari na raia, hofu ikawapotea,
Kwao kuwa manufaa, riziki kujipatia,
Vigumu kufanikiwa, rushwa ikivumiliwa !

Ubaguzi ukiingia, vyovyote unavyokuwa,
Kwa koo kuzingatia, au siasa zikawa,
Rehema hujisanzua, mbali na watu kukaa,
Mafanikio nadra, palipo na ubaguzi?

Upendeleo balaa, wa ndugu nao jamaa,
Kila unapoingia, hauachi kuchafua,
Vitu vyote kusinzia, hadi rivasi ikawa,
Vigumu kufanikiwa, palipo upendeleo !

Umbeya palipojaa, wema watapakimbia,
Ikabakia nazaa, mafuu pia vichaa,
Bure waliozoewa, riziki kujipatia,
Mafanikio nadra, umbeya palipojaa !

Kashfa zinapojaa, huota mkubwa waa,
Madoa yalotitia, kazi kweli kuyatoa,
Fisadi gamba kuvaa, uchafu ndani ukawa,
Vigumu kufanikiwa, kashfa zikifukiwa !

Haki ikununuliwa, sheria inalemaa,
Imani ikapotea, majaji kudharauliwa,
Na vyombo vikakimbiwa, watu peke kubakia,
Mafanikio nadra, haki ikinunuliwa !

Masikini wakiibiwa, husikitika dunia,
Na machozi ikatoa, haki kuwapigania,
Si kazi kujipindua, miguu juu ikawa,
Vigumu kufanikiwa, vya fakiri vikiliwa !


No comments: