Tuesday, June 12, 2012

Wanamitindo walafi



Yabadilika dunia, wengine hawajajua,
Wanataka kama kawa, ilivyo kuendelea,
Kwa wengi huu ni udhia, wanataka kuutoa,
Wanamitindo walafi, waifilisi dunia !

Watu wajishindilia, kama dona lilokuwa,
Katika kujenga njia, matumbo kuyanyanyua,
Na wenzao waumia, kwa kiu pia na njaa,
Wanamitindo walafi, waifilisi dunia !

Bilioni wazitwaa, kwa kuiga na sanaa,
Jasho wanaolitoa, kidunchu kuambulia,
Swali sasa latembea, sababu kuitambua,
Wanamitindo walafi, waifilisi dunia !

Ni fisadi walokuwa, bei wakaziinua,
Hali zao kutanua, na vifug kuvifua,
Hakuna la kuingia, ila gharama zajaa,
Wanamitindo walafi, waifilisi dunia !

Soka ukiangalia, wakubwa walitumia,
Chumo haramu kutwaa, vya wengi wakajilia,
Na maisha ya sanaa, na anasa kuogea,
Wanamitindo walafi, waifilisi dunia !

Na sinema nazo  pia, wengi zinawaibia,
Trilioni wazitwaa, ili kwenda jichafua,
Ndio ukiangalia, yanawaua madawa,
Wanamitindo walafi, waifilisi dunia !

Na muziki nao pia, hasa wao wa Ulaya,
Fedha wanazichukua, haramu zilizojaa,
Sauti kuandalia, watu wanararuliwa,
Wanamitindo walafi, waifilisi dunia !

Mipaka wamepitua, watakiwa kwangalia,
Na nafsi kuchungua, kama haki inakuwa,
Na kama wakijijua, hili watalikataa,
Wanamitindo walafi, waifilisi dunia !

Usawa unatakiwa, kugawa kinachoingia,
Isibweteke dunia, wengine kuwaachia,
Bilioni kuchukua, wengine kukosa mia,
Wanamitindo walafi, waifilisi dunia !

Haki hili halijawa, wataomba kulaaniwa,
Hasira zikiwajaa, hapa hamtapakaa,
Ni wapi mtakimbilia, msokwenda kujifia ?
Wanamitindo walafi, waifilisi dunia !

Twayataka manufaa, ya msingi kupatiwa,
Kisha watu kutumbua, na hekalu kunyanyua,
Vinginevyo twakataa, misuli tutazinoa,
Wanamitindo walafi, waifilisi dunia !

Mliua ujamaa, uroho mliojaa,
Hali fika mnajua, ubepari ni kinyaa,
Sasa mnajionea, kitu gani mwatwambia ?
Wasanii wenye shibe, waifilisi dunia !
Wanamitindo walafi, waifilisi dunia !

No comments: