Monday, June 18, 2012

T A N G A N Y I K A, T A N G A N Y I K A



WASOTAKA Tanganyika, yao wameshaamua,
Wayasema kwa mashaka, busara hawajajua,
Msiba utatufika, hilo lao kijakuwa,
Tanganyika, Tanganyika, hivi nani kaiua ?

Usanii wafanzika, uchama kuuridhia,
La umma kukatalika, azma yao ikawa,
Na Mola alimulika, hili ni vigumu kuwa,
Tanganyika, Tanganyika, hivi nani kaiua ?

Nchi zilizoungika, kitu kimoja kikawa,
Mzizi unaoshika, nchi mbili hutambua,
Ya tatu ikafanzika, ubia kuchaguliwa,
Mkiua Tanganyika, muungano utapona ?
Tanganyika, Tanganyika, hivi nani kaiua ?

Leo tumeathirika, moja imezainiwa,
Na watu wanapotaka, mizengwe wanafanyiwa,
Haudumu ushirika, usawa usiokuwa,
Tanganyika, Tanganyika, hivi nani kaiua ?

Kwa watu yahitajika, haki kuizingatia,
Na eneo kadhalika, kwa ukubwa kuridhia,
Na jambo likifanyika, adili yazingatiwa,
Tanganyika, Tanganyika, hivi nani kaiua ?

Nawajuza wasifika, mbele yatakayotokea,
Tanganyika mkizika, Tanzania mwaiua,
Moyoni sina mashaka, hili budi kuwafika,
Tanganyika, Tanganyika, hivi nani kaiua ?

Wapo waliotukuka, haya waliyakaa,
Na siku ilipofika, wote wameadhirika,
Urussi yalifanyika, leo tunajionea,
Tanganyika, Tanganyika, hivi nani kaiua ?

Kwa Tito mstahika, yalijiri Yugolavia,
Mauaji kufanyika, na udini kuuzua,
Bure mnahangaika, moto petroli mwatia,
Tanganyika, Tanganyika, hivi nani kaiua ?

Msingi haujajengeka, kuta mnakimbilia,
Nondo hamjaziweka, nguzo mnang'ang'ania,
Ni ajabu kuinjika, chungu bila ya mkaa,
Tanganyika, Tanganyika, hivi nani kaiua ?

Funguo tumezishika, katiba kuifungua,
Tuzungumze hakika,na kinani kuingia,
Ikibidi kufumuka, hayo yetu maljaliwa,
Tanganyika, Tanganyika, hivi nani kaiua ?

Tuyaondoe mashaka, vichwa vyetu kutulia,
Tuwe nayo ya hakika, yaafayo zungumzia,
Midomo ikifungika, uzaini twautia,
Tanganyika, Tanganyika, hivi nani kaiua ?


No comments: