Thursday, June 28, 2012

Wasanii watakiwa



Wengine hawatufai, twataka wenye sanaa,
Waitwao wasanii, ajira wakapatiwa,
Hadi ubunge kupewa, kuigiza kwa ridhaa,
Wasanii watakiwa, kujiunga nacho chama !

Haya ni yetu madai, rahisi twajiuzia,
Shazia pia na sui, sasa twajitafutia,
Huku tunapiga nai, mamluki kuchukua,
Wasanii watakiwa, kujiunga nacho chama !

Ni chama cha kitalii, hakina kinapotulia,
Huziwamba zake rai, ngoma ikajipigia,
Wetu si wa baibui, nusu uchi wanakaa,
Wasanii watakiwa, kujiunga nacho chama !

Ihsani hawajui, kidogo kinawanunua,
Na wazee si nishai, bei poa twachukua,
Ni sadaka ya jamii, hili tumeshajaliwa,
Wasanii watakiwa, kujiunga nacho chama !

Hapana istizahi, wala wa kuwatania,
Hapajawa makuruhi, hishma kuichafua,
Hii ya haki bei, watu tunaponunua,
Wasanii watakiwa, kujiunga nacho chama !

Kazi yao usanii, kuiga na kuingia,
Kwetu kama makarai, maji budi kuyatia,
Bafuni kuleta uhai, pale tunapojiogea,
Wasanii watakiwa, kujiunga nacho chama !

Watakiwa wasanii, chamani kuja ingia,
Wakaigiza futuhi, bungeni wakijakaa,
Wananchi kufurahi, wakasahau udhia,
Wasanii watakiwa, kujiunga nacho chama !

Kama nazi nalo tui, hudamka kitumbua,
Juu ukitia chai, staftahi itakuwa,
Na andazi sikinai, na urojo nao pia,
Wasanii watakiwa, kujiunga nacho chama !

Watu hawawatambuia, na yao yanayowafaa,
Na pale wanapozirai, wadhani wawazimia,
Na makwetuhawakai, vipi yetu kuyajua ?
Wasanii watakiwa, kujiunga nacho chama !

Yawanogea tivii, na sura kujionea,
Hata wasipo na rai, upuuzi kuongea,
Inawatia nishai, nje wakiongelewa,
Wasanii watakiwa, kujiunga nacho chama !

Vidonda hawaondoi, daima huviachilia,
Sasa inarudi ndui, sanaa yaendelea,
Na ukimwi wajiwahi, fedha wajipukuchulia,
Wasanii watakiwa, kujiunga nacho chama !

No comments: