Sunday, June 17, 2012

Meli tunayosafiri



Wajifanyao jeuri, na kiburi kujitia,
Ninawapasha habari, meli tuliyoingia,
Ni ya kwetu manowari, moja tunayotumia,
Meli tunayosafiri, moja, MV Tanzania !

Katikati ya bahari, ya hii yetu dunia,
Tukiwamo twasafiri, tunapaswa kutambua,
Iwe heri, iwe shari, bado moja yetu njia,
Meli tunayosafiri, moja, MV Tanzania !

Yatupasa tafakari, kila tunaloamua,
Yetu kufanza shauri, maamuzi kuyajua,
Vinginevyo ni hatari, hata nahodha ukiwa,
Meli tunayosafiri, moja, MV Tanzania !

Safari ina hatari, na majanga ya blaa,
Watekaji waabiri, baharini wamejaa,
Nia yao sio nzuri,waweza tuingilia,
Meli tunayosafiri, moja, MV Tanzania !

Kuchukua tahadhari, yafaa kuzingatia,
Mabaharia hodari, lazima kuajiriwa,
Sio watu wa hiari, kazi wasioijua,
Meli tunayosafiri, moja, MV Tanzania !

Tukiianzisha shari, wote tutaangamia,
Haramia wakijiri, wote wakatuchambua,
Sote wakatuadhiri, na   vyetu kutuibia,
Meli tunayosafiri, moja, MV Tanzania !

Kwenye meli kuna chori, inafaa kuwajua,
Na hawa sio kachori, tofauti kuijua,
Hawa ni watu hatari, ni wezi wa kuzaliwa,
Meli tunayosafiri, moja, MV Tanzania !

Wajifanya wasafiri, usiku wakingojea,
Kisha wakazusha shari, na vitimbi kuvitia,
Watu kutia kabari, au meli kupindua,
Meli tunayosafiri, moja, MV Tanzania !

Ya mapenzi manowari, hii yetu yatakiwa,
Tusifanziane shari, mitegoni kuingia,
Ikatukimbia heri, mashakani kuingia,
Meli tunayosafiri, moja, MV Tanzania !


No comments: