Monday, June 18, 2012

Hongereni Chama



Asante chama tawala, kwa vilabu na malaya,
Tabata ni halahala, sasa hivi twavamiwa,
Kama hutaki kulala, njoo vingine potea,
Hongereni chama hiki, kwa kuifanya Tabata,
Kama vile Kinondoni,
Kwa pombe na Changudoa !

Tumefanyiwa fadhila, kuenezewa mabaa,
Hii sio kama lila, ni yetu njema hidaya,
Tunaliwa, tunakula, wala hakuna umbeya,
Hongereni chama hiki, kwa kuifanya Tabata,
Kama vile ni Ohio,
Kwa pombe na Changudoa !

Kata yetu ni jalala, kila kitu twatupiwa,
Tumezawadiwa  hila, ili kizazi kuvia,
Unajua utawala, kibali waliotoa,
Hongereni chama hiki, kwa kuifanya Tabata,
Kama vile Kinondoni,
Kwa pombe na Changudoa !

Wengine juu walala, chamani wametulia,
Na kura wameshakula, japo kwa kutuibia,
Wakishazipata hela, nasi hatutawafukia,
Hongereni chama hiki, kwa kuifanya Tabata,
Kama vile ni Ohio,
Kwa pombe na Changudoa !

Wajifie kama swala, porini walikokuwa,
Funza wapate kuwala, mchangani kuishilia,
Hiyiondiyo yetu sala, nyingine hatutaijua,
Hongereni chama hiki, kwa kuifanya Tabata,
Kama vile Kinondoni,
Kwa pombe na Changudoa !

Kwa kweli ni kama swila, watu hawa nawambia,
Simu yao ina dola, hakuna wasilojua,
Kuua kwao ni mila, ukwasi  kuufatia,
Hongereni chama hiki, kwa kuifanya Tabata,
Kama vile ni Ohio,
Kwa pombe na Changudoa !

Katuambia Makilla, mtunzi alojaliwa,
Mola amtunze Mashallah, kwa ukweli kuutoa,
Ajua bila jamala, italia Tanzania,
Hongereni chama hiki, kwa kuifanya Tabata,
Kama vile Kinondoni,
Kwa pombe na Changudoa !

Haya ndio masuala, watunzi kuzungumzia,
Kajitoeni kafala, haya kuyasabiia,
Kafiri wana madhila, imani zatupotea,
Hongereni chama hiki, kwa kuifanya Tabata,
Kama vile ni Ohio,
Kwa pombe na Changudoa !



No comments: