Sunday, June 17, 2012

Hayat Bob Makani



Inna lillahi waina illahi rajiuuni,
Bob Makani hatuna, kaondoka muumini,
Twamuombea Rabana, ampe yake hisani,
Hayati Bob Makani, kalale pema peponi !

kaondoka duniani, baada ya udhamini,
CHADEMA  kuiauni, na kuijenga makini,
Sasa ni chama cha kuwini, kutawala mjengoni,
Rejeo ni kwa Manani, viumbe wa duniani,

Heshima yake kuwini, budi kwenda vijijini,
Huko ndiko mizizini, kwenda ijenga imani,
Wajue yake amini, kuwatoa mashakani,
Hayati Bob Makani, kalale pema peponi !

Tumebaki duniani, kuwafaa masikini,
Pia nao waumini, watokao kila dini,
Wote sisi kwa imani, mmoja twamuamini,
Hayati Bob Makani, kalale pema peponi !

Watu  hawakuwazaini, ili yake waamini,
Awafanzie utani, wakaikosa amani,
Hakuitoa yakini, lililo kuwa shakani,
Hayati Bob Makani, kalale pema peponi !

Ni Gavana wa zamani, kaishi kimaskini,
Ufisadi kauhini, akaijenga imani,
Hakuongeza madeni, nchi kuwa taabani,
Hayati Bob Makani, kalale pema peponi !

Kayaingiza chamani, vijana kuwaamini,
Kawatilia ubani, wawe safi waumini,
Wasiwe kama wahuni, tuwajuao nchini,
Hayati Bob Makani, kalale pema peponi !

Kakaa nao kundini,kuwapa wake undani,
Waende namna gani, watu wakawathamini,
Ikiwa hapa mjini, pia huko vijijini,
Hayati Bob Makani, kalale pema peponi !

Muulize Freeman, mwalimu kamuamini,
Zitto kwenda ughaibuni, ushauri kauthamini,
Tundu kijana makini, anawafunza bungeni,
Hayati Bob Makani, kalale pema peponi !

Na ishara zote nchini, watu wanawamini,
Wengi wao wanadhani, wengine ni watu duni,
Kushika nchi mwakani, hawa ni kuwadhamini,
Hayati Bob Makani, kalale pema peponi !

Ameondoka Makani, kaacha chama makini,
Ikishachorwa ramani, na vijiji kuauni,
CHADEMA wakaamini, ndio yao afueni,
Hayati Bob Makani, kalale pema peponi !

Atafurahi Makani, alofanza duniani,
Tukamlipa hisani, matunda kwa kuyawini,
Demokrasia nchini, isiwe tena shakani,
Hayati Bob Makani, kalale pema peponi !

Mtimizie Manani, huyu wako Muumini,
Ya ukweli kaiamini, moja kwa moja peponi,
Na wajue muumini, chama hakina udini,
Hayati Bob Makani, kalale pema peponi !



No comments: