Monday, June 18, 2012

Utamsahau ?



KILA mtu awajua, yeye tunamshangaa,
Ushoga kauingia, mchana uliokuwa,
Heri akiitazamia, kwingine 'sikotokea,
Hivi utamsahau,kula naomumiani ?

Na taasisi kadhaa, na wengine kugaia,
Misaada kuitwaa, ili wakajishibia,
Na kila mwenye kujua, zimwi ameshaingia,
Hivi utamsahau, kunywa nao chinjachinja ?

Upofu wamewatia, na uziwi nao pia,
Yamekwisha majaliwa, dhahabu kugnguliwa,
Ndani ameshakaa, kumtoa ataua,
Hivi utamsahau, kula naomumiani ?

Tabasamu kajaliwa, kulemaza na kuua,
Kila nikiangalia, sioni pakutokea,
Na vikosi vyaingia, uhasama kuja zua,
Hivi utamsahau, kunywa nao chinjachinja ?

Safari zilizokuwa, puani kututokea,
Na uongo wakazua, yao kuja kuwafaa,
Marafiki watajaa, maadui walokuwa,
Hivi utamsahau, kula naomumiani ?

Saini wamezitia, ya kwetu kutuibia,
Ni kushoto na kulia, hapana palipobakia,
Mumiani waingia, damu kuja jinyonyea,
Hivi utamsahau, kunywa nao chinjachinja ?

Vya neti wanajilia, vya ukimwi vyafatia,
Uongo na  kweli huwa, yote wanojifanzia,
Salama yao hadaa, kuna yao kutimia,
Hivi utamsahau, kula nao mumiani ?

Tumezizua sheria, watu wetu kuwagawa,
Wakubwa wanunuliwa, haki wanaziachia,
Mfukoni wametiwa, kutoka ninahofia,
Hivi utamsahau, kunywa nao chinjachinja ?

Oneni yanayotokea, kwa pipi mnazopewa,
Dhahabu wanachukua, kila kitu mwaachia,
Ufukara mwajitia, muombe kusaidiwa ?
Hivi utamsahau, kula nao mumiani ?

Huu mkubwa mzaha, masikini Tanzania,
Ombaomba tunakua, utajiri umejaa,
Akili tumelemaa, na watu tunatumiwa?
Hivi utamsahau, kunywa nao chinjachinja ?

Wakubwa tunateua, waliozidiwa njaa,
Makombo wakipatiwa, waona wamejaliwa?
Pasi aibu wala haya, wasema tumeendelea?
Hivi utamsahau, kula nao mumiani ?

Sahau haitakuwa, kumbukumbu zitakaa,
Uhai wakijaliwa, wenyewe kujionea,
Na watu wakaamua, nini cha kuwafanzia,
Hivi utamsahau, kunywa nao chinjachinja ?

Balaa kuiondoa, dua zetu zatakiwa,
Kila siku, kila saa, Mola tuwe twamlilia,
Hupangwa akapangua, naye njia anazijua,
Hivi utamsahau, kula nao mumiani ?

No comments: