Monday, June 18, 2012

Ukicheza na mbwa



ACHA na mbwa kucheza, asije kukuchezea,
Bila ya kukuuliza, msikitini huingia,
Keshakuona ni mwenza, kucheza ajisikia,
Ukicheza na mbwa, msikitini huingia !

Kuna watu wa kuoza, kazi yao kutumiwa,
Heri hata ya mafunza, wanajua pa kukaa,
Hawa si wa kufunzwa, utu kwao ni kinyaaa,
Ukicheza na mbwa, msikitini huingia !

Akili zao huviza, haki kutoitambua,
Wakayameza ya viza, kutupwa yanayofaa,
Ukweli huwa waiza, wanajali manufaa,
Ukicheza na mbwa, msikitini huingia !

Shere bila kuwacheza, wewe watakuchezea,
Ngoma ukiituliza, na akili kufungua,
Jibari huwamaliza, neno wakalielewa,
Ukicheza na mbwa, msikitini huingia !

Njaa tuu inawauza, si watu wa kujitambua,
Na wakizuka waweza, riziki wakawapatia,
Ya wengine wakaiza, yako wakayasikia,
Ukicheza na mbwa, msikitini huingia !

Na huu si muujiza, ujanja wanaujua,
Upacha wanauteza, huku na huku kufaa,
Na zao lao hukuza, mara mbili kuja kuwa,
Ukicheza na mbwa, msikitini huingia !

Mbwa ukishamfunza, mlinzi huweza kuwa,
Akulinde si kubeza, kazi akajifanzia,
Na wewe ukamtunza, yeye kukuangalia,
Ukicheza na mbwa, msikitini huingia !

Chema kweli chajiuza, hivi nani asojua,
Kibaya chajitembeza, kwa thamani kupungua,
Hata nawe ni muweza, hili waweza tatua,
Ukicheza na mbwa, msikitini huingia !

No comments: