Sunday, June 17, 2012

Urais nalilia


Jamani mngelijua, nchi mngeniachia,
Nina zangu ruia, zatakiwa kutimia,
Rais nisipokuwa, madeni yataniua,
Urais nalilia, ndoto zangu kutimia !

Sina uchu nawambia, ila nimeandikiwa,
Lakini inatakiwa, nyie kunisadia,
Na shilingi nazitoa, milango kuifungua,
Urais nalilia, ndoto zangu kutimia !

Uroho nimekataa, ili hiwa yangu hawa,
Hamjui ninajua, kutoka na kuingia,
Urais kwangu hewa, bilayo siwezi pumua,
Urais nalilia, ndoto zangu kutimia !

Ulafi sikujaliwa, ila watu kutumia,
Kisha nikawachafua, ya kwangu kufanikiwa,
Na vidonge navitoa, dawa na visivyo dawa,
Urais nalilia, ndoto zangu kutimia !

Watu watanikimbia, rais nisipokuwa,
Muhibu ninahofia, hata naye yumo pia,
Kwangu kizaazaa, siombi likatokea,
Urais nalilia, ndoto zangu kutimia !

Dishi limeepuliwa, mezani linaingia,
Na wa kwanza kupakuwa, ni mimi ninatakiwa,
Wengine kuwazuia, swahibu mnatakiwa,
Urais nalilia, ndoto zangu kutimia !

Magazeti nanunua, redio, tivii pia,
Sura yangu kutumia, ila nisiposinzia,
Magari mtapatiwa, hata juu mkapaa,
Urais nalilia, ndoto zangu kutimia !

Machiavelli radhia, ushauri natumia,
Hulazimika kuua, Macbeth anajua,
Ufalme kuutwa, mizuka kutohofia,
Urais nalilia, ndoto zangu kutimia !

Urais ni tabia, haiba na kujongea,
Siwezi kukata nia, labda sijazaliwa,
Gele wanaonionea, nyota hawatatungua,
Urais nalilia, ndoto zangu kutimia !


No comments: