Thursday, June 14, 2012

Jimbo hili nimepewa



Mimi piwa mswahili,  Manani kanijalia,
Ni lugha yangu asili, toka nilipozaliwa,
Hata sasa nahimili, umma kuuandikia,
Jimbo hili nimepewa, Kiswahili kukilinda !

Ninaiona kamili, utajiri imejaa,
Hii lugha ya halali, haramu yaukataa,
Kwangu ni kama kandili, njia yaniangazia,
Jimbo hili nimepewa, Kiswahili kukienzi !

Inaweza ya awali, na ya akheri yakawa,
Rijali na wanawali, kwa yote kuwaandaa,
Wakifika ngazi ya pili, lugha ngeni wakajua,
Jimbo hili nimepewa, Kiswahili kukijenga !

Watoto wana akili, lugha haitochentua,
Waweza wasome mbili, hata na ya tatu pia,
Ya msingi mahafali, ikwa tatu wajua,
Jimbo hili nimepewa, Kiswahili kukijenga !

Na hiyo ngazi ya pili, kazini wanapokuwa,
Ili kufata ya mbali, wapaswayo kuyajua,
Waende kuyanakili, kwa Kiswahili yakawa,
Jimbo hili nimepewa, Kiswahili kukilinda !

Wachina hili wajali, yote sasa wanajua,
Hao ni watu kamili, si nusu waliokuwa,
Sisi bado ni kivuli, utu hatujatambua,
Jimbo hili nimepewa, Kiswahili kukienzi !

Amkeni bilkuli, majimboni mlojaa,
Bongo zijibu maswali, lugha ipi kutumia,
Hali wa kwenda mbali, Kichina budi kujua,
Jimbo hili nimepewa, Kiswahili kukijenga !

Kiarabu afadhali, herufi tukipindua,
Mwandiko wa Kiswahili, hazina itafukua,
Ama sabini na mbili, yatimu asilimia,
Jimbo hili nimepewa, Kiswahili kukilinda !

Maneno ya Kiswahili, Kiarabu yalokuwa,
Ukifanza udahili, kamusii mbili watoa,
Jamani hii si mali, yatosha kujifunzia ?
Jimbo hili nimepewa, Kiswahili kukienzi !

Nilishasema awali, hadimu hatojaliwa,
Ili kulikabili, na kweli likatokea,
Alaa, hii ndiyo hali, nchini najionea,
Jimbo hili nimepewa, Kiswahili kukijenga !


No comments: