Wednesday, July 18, 2012
FIDIA YETU UHUNI
Ndio ma'na wanaua, fidia zetu dhihaka,
Maisha ya Mtanzania, thamani hatujaweka,
Vishilingi twalipia, mpewa akajicheka,
Fidia zetu dhihaka, ndio ma'na tunaaua !
Watazungumza wanaa, na Mola kumzulia,
Ila wa mtu ukiwa, mkono tunaujua,
Muhyi huwasaidia, wanaojisaidia,
Fidia zetu dhihaka, ndio ma'na tunaaua !
Tajiri watutania, ni wa kufa na kuzika,
Thamani waitambua, milioni kutofika,
Vijisenti watambua, hawawezi pepesuka,
Fidia zetu dhihaka, ndio ma'na tunaaua !
Wakubwa wamewatia, mfukoni kuwaweka,
Yao wanayaelewa, wana njaa za kunuka,
Nani wa kuwatishia, thamani kuongezeka ?
Fidia zetu dhihaka, ndio ma'na tunaaua !
Mahakama wazishika, rahisi zitaamua,
Hawawezi filisika, biashara kwendlea,
Wao hawana mashaka, ni Mungu ameamua !
Fidia zetu dhihaka, ndio ma'na tunaaua !
Hawa ni Waafrika, ndiyo yao kugundua,
Ukija umefyatuka, yaweza kukutokea,
Bila kanuni kuweka, na wageni watalia,
Fidia zetu dhihaka, ndio ma'na tunaaua !
Safari zetu mashaka, na ajali majaliwa,
Tajiri hatoteseka, masikini huumia,
Kisha huzuka vizuka, ya uongo wakalia,
Fidia zetu dhihaka, ndio ma'na tunaaua !
Wanga watadaamka, na machozi kuyatoa,
Kumbe wao ndo mahoka, kisa kilichochangia,
Maiti wakasifika. pengo wametuachia,
Fidia zetu dhihaka, ndio ma'na tunaaua !
Pengo likaelezeka, na wasifu kuutoa,
Hawawezi kuzuzuka, kazi wameizoea,
Ya mnyonge patashika, ndiyo aliyojaliwa,
Fidia zetu dhihaka, ndio ma'na tunaaua !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment