Wednesday, July 18, 2012
Wanautaka ukubwa
WASUMBUKAO kwa njaa, ya ukubwa kuukwaa,
Fumbo nimelifumbua, kuongoza hufulia,
Wakawa wang'ang'ania, watu huku waumia,
Wanautaka ukubwa, kuongoza hawawezi !
Njaa yao kutumbua, vya umma wakajilia,
Wala si kusaidia, na watu kuwanyanyua,
Yao wamedhamia, siye nyie kuwafaa,
Wanautaka ukubwa, kuongoza hawawezi !
Ukubwa wanadhania, ni nafasi kuchukua,
Kichwani wakawa wang'aa, kwa utupu kuuvaa,
Hawana la kuamua, la wananchi kuwafaa,
Wanautaka ukubwa, kuongoza hawawezi !
Ni mzigo wanakuwa, mabegani mwa raia,
Badala kuendelea, huwa tunadidimia,
Lakiini watajisifia, eti twapiga hatua,
Wanautaka ukubwa, kuongoza hawawezi !
Kaitazame Malaysia, au nayo Indonesia,
Udhia utatambua, na dhihaka kuagua,
Kila mwenye kujisifia, kasoro nyingi kajaa,
Wanautaka ukubwa, kuongoza hawawezi !
Vya msingi twaachia, ugaidi tunalia,
Ya kwetu twayaachia, ya wazungu kuchukua,
Ila si yanayofaa, bali wao kuridhia,
Wanautaka ukubwa, kuongoza hawawezi !
Juu wanakobakia, ndiko wanaishilia,
Ya chini hawatajua, uongo watagawiwa,
Ajizi kupakuliwa, wakala na kucheua,
Wanautaka ukubwa, kuongoza hawawezi !
Ujinga unatuua, ya kwetu kutotambua,
Haya yanapotokea, watu tunawaaachia,
Na Mungu kumzulia, ya shetani yalokuwa,
Wanautaka ukubwa, kuongoza hawawezi !
Shetani achekelea, Mola kumsingizia,
Na namba anatutia, wajihini zikang'aa,
Hakika tutakijua, nachelea, nahofia,
Wanautaka ukubwa, kuongoza hawawezi !
Tupe nafuu jalia, uongozi wa kufaa,
Hali kuzia.ngalia, na kupungua nazaa,
Tuvute kukurudia, tukakimbia hadaa,
Wanautaka ukubwa, kuongoza hawawezi !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment