Wednesday, July 18, 2012
Z A N Z I B A R, Z A N Z I B A R !!!
Inna lillahi Alaa, waina illahi rajiuuni,
Visiwani tunalia, kwa kukosa tumaini,
Kila siku kufiliwa, kwenye njia baharini,
Zanzibar, Zanzibar, kila siku tunalia !
Ajali tumezoea, sera mpya twazibuni,
Kwa ajizi na udhia, nchi wamesharubuni,
Wenye fedha waachiwa, leseni za mumiani,
Zanzibar, Zanzibar, kila siku tunalia !
Ndugu ninawalilia, inaniuma moyoni,
Pole yao nakataa, naona kama uhuni,
Tunaweza kuzuia, amini usiamini,
Zanzibar, Zanzibar, kila siku tunalia !
Eti meli zatembea, ofisi hatuzioni,
Au ni za Liberia, au kutoka Japani,
Seagull yaelea, wenye mali kina nani?
Zanzibar, Zanzibar, kila siku tunalia !
Mitumba twaitumbua, nayo yatufanyanini?
Ndiyo sera na sheria, kukwaa na kujihini,
Kuna watu wachangia, twamsingizia shetani ?
Zanzibar, Zanzibar, kila siku tunalia !
La bidanamu kavaa, huyo jini mumiani,
Na uhuru amepewa, kuufanya uhaini,
Ndani nje kuchungua, yasifichwe asilani,
Zanzibar, Zanzibar, kila siku tunalia !
Fidia zetu nazaa, zinatushusha thamani,
Ndio ma'na inakuwa, wanakosa umakini,
Kitu kidogo wakiipewa, twaumia masikini,
Zanzibar, Zanzibar, kila siku tunalia !
Jalali twakulilia, kwa adha na usononi,
Ndiye uliyebakia, viumbe wavithamini,
Tulioishawachagua, wametuacha mataani,
Zanzibar, Zanzibar, kila siku tunalia !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment