Wednesday, July 18, 2012

Mnyonge ana sauti






WAO ni kama maiti, nani wa kuangalia,

Waliokalia viti, mengine yawasumbua,

Mnyonge hana bahati, kaziye kuhujumiwa,

Mnyonge ana sauti, ushairi kupitia !



Hukisiwa afriti, mengi akitumumiwa,

Hata ndugu humsaliti, jaha kuikimbilia,

Akaishia makuti, na donge la kukandia,

Mnyonge ana sauti, ushairi kupitia !



Ya kwake hawayateti, wala kuzungumzia,

Yakitiwa kwenye hati, msaada watakiwa,

Fukara haumkuti, mifukoni huishia,

Mnyonge ana sauti, ushairi kupitia !



Wala hanayo kamati, yake yakafikiriwa,

Hakuna ya kweli dhati, umaskini kutoa,

Mambo yao hatihati, wenyewe kujipalilia,

Mnyonge ana sauti, ushairi kupitia !



Fukara haumkuti, mifukoni huishia,

Kwa wenye kuvaa suti, na ghorofa za kofia,

Maskini kibushuti, hana anachoambulia,

Mnyonge ana sauti, ushairi kupitia !



Mnyonge hana bahati, kaziye kusahauliwa,

Au kama kibiriti, hutumika kuwashia,

Na mezani hakiletwi, mtu kikishamfaa,

Mnyonge ana sauti, ushairi kupitia !



Ni mtumwa wa vicheti, na vya bure vibarua,

Zoezini humkuti, ila kwenye kuhesabiwa,

Anazo nyingi shuruti, vizuri kutawaliwa,

Mnyonge ana sauti, ushairi kupitia !



Mwanaye hali biskuti, wala kupewa halua,

Daraja la pili si kati, hilo kaishachaguliwa,

Hata akiwa 'smati', ndipo hapo huishia,

Mnyonge ana sauti, ushairi kupitia !



Yananiuma magoti, nashindwa kuendelea,

Ila wasia wa dhati, huu nishawaambia,

Mazuri hatuyakuti, mnyonge tumimuonea,

Mnyonge ana sauti, ushairi kupitia !



Mshairi siwasaliti, nazidi kuwatetea,

Hadi nipate mauti, na wengine kuachia,

Namuomba Muqsiti, daima kuangalia,

Mnyonge ana sauti, ushairi kupitia !

No comments: