Thursday, December 1, 2011

Uganga ukishaisha

Uganga ukiishia ubwana unapotea,
Na nguvu ukaishiwa, utoto ukarudia,
Hata uliyoyajua, yaja tena kupotea,
Uganga ukishaisha, inabaki kufulia.

Shiriki mwana hadaa, koja bovu la dunia,
Na wanaoitegemea, huishia kusinyaa,
Ahadi akiamua, kila kitu huchukua,
Uganga ukishaisha, inabaki kufulia.

Nipe lenye manufaa, imani isiyochakaa,
Mmoja kumwaminia, mlinzi anayefaa,
Mchana nikitembea,na usiku nikisinzia,
Uganga ukishaisha, inabaki kufulia.

Naikimbia sanaa, shetani anayojua,
Mbali naye nikakaa, na Mola kumtegemea,
Na ninaowaridhia, wapaswa hili kujua,
Uganga ukishaisha, inabaki kufulia.

No comments: