Saturday, December 29, 2012

Tulicho nacho kutunza



Vipi twaweza kutunza, bila kidogo kwanzia,
Hapa tulipojibanza, panafaa kuanzia,
Hiki tusipokitunza, kikubwa huwa fadhaa,
Tulicho nacho kutunza, lazima tukithamini!

Vichaa wakiapiza, yao kutoyasikia,
Kila kitu kina kwanza, kwa hatua kikakua,
Wanaotaka kufanza, haraka watindikiwa,
Tulicho nacho kutunza, lazima tukithamini!

Mambo yataka kukweza, kwa ngazi kujipandia,
Yakiwa ni ya kutweza, kupaa hukuumbua,
Mwatakiwa kuyaweza, kwa kanuni na sheria,
Tulicho nacho kutunza, lazima tukithamini!

Ruia wanaopaaza, hao wa kuangalia,
Wanaweza kuwakwaza, na sio kuendelea,
Kisha waje kuwaponza, mlicho nacho kwishiwa,
Tulicho nacho kutunza, lazima tukithamini!

No comments: