Saturday, December 29, 2012
Mpaji na mnyang'anyaji
NDIYE mwenye kugawiwa, wengi wasema kutoa,
Kisha akaja kutwa, vyake akavihukua,
Nani wa kumchezea, sahihi aliyekuwa ?
Mpaji na mnyang'anyaji, huyo huyo si mwingine !
Ni mwepesi wa kutoa, kiumbe ukajaliwa,
Nyota yako juu kuwa, ikunukuu dunia,
Wajibuo ukijua, hapo waweza bakia,
Mpaji na mnyang'anyaji, huyo huyo si mwingine !
Mrahisi kuachia, kama ya kushikilia,
Weye kujishtukia, chini unaangukia,
Na unapotumbukiwa, humohumo ukakaa,
Mpaji na mnyang'anyaji, huyo huyo si mwingine !
Akiependa kwa ridhaa, aweza akakutoa,
Fursa kukuachia, upendavyo kutumia,
Ukawa wako wasaa, kuzama au kupaa,
Mpaji na mnyang'anyaji, huyo huyo si mwingine !
Wengi wanapogawia, huanza kujizuzua,
Njia wakaiachia, na kuingia nazaa,
Pasina ya kuelewa, kwao hakuna wasaa,
Mpaji na mnyang'anyaji, huyo huyo si mwingine !
Na anavyoshudhudia, kifua mnakiinua,
Pindi mnapojaliwa, mazuri yanu yakawa,
Mkawa mwajisifia, yeye awapendelea,
Mpaji na mnyang'anyaji, huyo huyo si mwingine !
Kikija kuondolewa, hamtoacha kulia,
Udhalili kawatia, wapi mtakimbilia,
Kama vile mwajijua, nyie wa juu tu kukaa,
Mpaji na mnyang'anyaji, huyo huyo si mwingine !
Wajane hamkuwafaa, na yatima mwakimbia,
Masikini nao pia, yenu waliyahofia,
Hivi mkijichungua, haki hamjatendewa ?
Mpaji na mnyang'anyaji, huyo huyo si mwingine !
Kadari tungeliijua, hivi tusingelikuwa,
Mengi tungeyaachia, na machache kufatia,
Wengi tunachokimbilia, wala hatutachukua,
Mpaji na mnyang'anyaji, huyo huyo si mwingine !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment