Saturday, December 29, 2012

SI UKUU HUU



KATIKA hii miaka, ya ujanja na hadaa,
Jambo ninalolijua, uchaguzi watakiwa,
Watu wakamchagua, kiongozi wa mkoa,
Si ukuu wa mkoa, nchi utakaojenga!

Kwenye mwaka wa fadhaa, ukweli tutapojua,
Uongo tukifaragua, na ukweli kuenea,
Nchi umoja kulea, lazima huru mikoa,
Si ukuu wa mkoa, nchi utakaojenga!

Nchi tuanjionea, vidogo vilivyokuwa,
Guinea Equatorial, milioni hawajawa,
Chumo wanajichumia, mkuu akachezea,
Si ukuu wa mkoa, nchi utakaojenga!

Dubai haijafikia, ya kwetu mingi mikoa,
Mauritius nayo pia, na Seychelles nakwambia,
Ila wanazitungua, hazinani kuingia,
Si ukuu wa mkoa, nchi utakaojenga!

Bahrain angalia, na Brunei nako pia,
Ka-Qatar ukijua, hautoyaridhia,
Ya kati kutawaliwa, watu wasikofikiwa,
Si ukuu wa mkoa, nchi utakaojenga!

Ili uchumi kukua, njia ni huru mikoa,
Yao wakayaamua, kupanga na kupangua,
Rasilimali zikawa, zinaufaa mkoa,
Si ukuu wa mkoa, nchi utakaojenga!

Wengine wakatambua, umuhimu watakiwa,
Za kwao kuzichumbua, pia nao kuwafaa,
Kubebana sio dawa, pua tutaangukia,
Si ukuu wa mkoa, nchi utakaojenga!

Mtu huru atakiwa, maamuzi kuyatoa,
Kisha akazingatia, utaifa kuufaa,
Mkoa kama nyumba huwa, kwanza kutolala njaa,
Si ukuu wa mkoa, nchi utakaojenga!

Yote kuichukulia, kama sawa imekua,
Ni siasa zenye njaa, katu hazitatufaa,
Mikoa kujitambua, hatuwezi likataa,
Si ukuu wa mkoa, nchi utakaojenga!

Mikoa kujitambua, fursa zilizokuwa,
Njia wakazichagua, za wao kuendelea,
Sawa haitatokea, tofauti itakuwa,
Si ukuu wa mkoa, nchi utakaojenga!

Haya tukiyaelewa, nchi tutaiimua,
Hamira tukaitia, ikaanza jifutua,
Kuoka rahisi kuwa, na vitamu kuzaliwa,
Si ukuu wa mkoa, nchi utakaojenga!

Umoja kuendelea, wala lhautajifia,
Ujerumani ni njia, hii waliyopitia,
Mtai anaijua, huko tulitembelea,
Si ukuu wa mkoa, nchi utakaojenga!

UJimbo sio balaa, bali sasa ndio njia,
Kenya wameshaamua, kwa ukabila twajua,
Sisi tumeendelea, bado tunalihofia ?
Si ukuu wa mkoa, nchi utakaojenga!

Ninaona ni hadaa, uchama kuendelea,
Wanachohofia, kuipoteza mikoa,
Upinzani kuitwaa, haraka ikajapaa,
Si ukuu wa mkoa, nchi utakaojenga!

Naanika si kuanua, wenyewe mtalijua,
Uchama kwetu tanzia, kifo unatuletea,
Ustawi unavia, hali wanajisifia,
Si ukuu wa mkoa, nchi utakaojenga!

Njaa yazidi kolea, shibe wanasimulia,
Kisha wanatushangaa, njaa kuitangazia,
Kwao sasa ni sanaa, mchezo wa kugiziwa,
Si ukuu wa mkoa, nchi utakaojenga!

No comments: