Saturday, December 29, 2012

ASIYEJUA SHABAHA


Huhangaika mkiwa, na hii kubwa dunia,

Shabaha aliyepwaya, hawezi akapatia,

Kila akifikiria, pengine atatungua,

Asiyejua shabaha, halengi  mpaka kufa!

 

Wengi nimeshuhudia, ujanja walijitia,

Kwa kiburi kujitia, kulenga wamesomea,

Ila kilichofatia, washinda kushuhudia,

Asiyejua shabaha, halengi  mpaka kufa!

 

Karibu waliyaachia, mbali wakayazuikia,

Kuja kutahamakia, mkenge wameingia,

Na walilolidhania, kama kweli halikuwa,

Asiyejua shabaha, halengi  mpaka kufa!

 

Kwa pembeni wafulia, ukutani  kuingia,

Kulalama wabakia, pengine wamechezewa,

Au wamehujumiwa, wala haki haikuwa,

Asiyejua shabaha, halengi  mpaka kufa!

 

Kilio watakizua, machozi wakayatoa,

Macho yaliathiriwa, uchafu ukaingia,

Au homa kuingia, ghafla mwili kulewa,

Asiyejua shabaha, halengi  mpaka kufa!

 

Yote ukiangalia, mwee, wanasingizia,

Ziliwazidi tamaa, huku na huku kwingia,

Saa ilipofikia, wkadhindwa kuamua,

Asiyejua shabaha, halengi  mpaka kufa!

 

Ndiyo yanayotokea, kwa wengi wa Tanzania,

Kwa walilojitakia, kuwa limewakataa,

Na walilolichukia, ndio sasa lawafaa,

Asiyejua shabaha, halengi  mpaka kufa!

 

Wapo walioolewa, hali ni bahati mbaya,

Mme mpenzi hajawa, na mkewe aidha pia,

Wanauzusha ubia, subira na kuvumilia,

Asiyejua shabaha, halengi  mpaka kufa!

 

Hawezi kushangaa, DNA yachukiwa,

Kwa kuizua balaa, na kweli ikazagaa,

Walio na maridhia, mkono hawajajaa,

Asiyejua shabaha, halengi  mpaka kufa!

 

Bwanangu mwenye kujua, neno ninakuachia,

Siri yangu waijua, na vyangu vilivyokuwa,

Asante kwa kuridhia, haki yangu kuipewa,

Asiyejua shabaha, halengi  mpaka kufa!

 

Wivu sitajionea, wenye vyao visokuwa,

Kidogo nilichopewa, kinaweza kunivua,

Subira nitailewa, pasina kulewa dunia,

Asiyejua shabaha, halengi  mpaka kufa!

No comments: