Saturday, December 29, 2012

Maneno tumeshashiba



KUSHIBA hamkuchelewa, ukubwa mlipopewa,
Vipit mwatutarajia, sisi tuwe twangojea ?
Mwenye shibe nimejua, hamjui  mwenye njaa,
Maneno tumeshashiba, tuna njaa ya vitendo.

Watu wamevumilia, sasa wajitapikia,
Nusura wakingojea, miaka ikaishia,
Uzee wakaingia, na wengine kujifia,
Maneno tumeshashiba, tuna njaa ya vitendo.

Wachoka Watanzania, wachche kujishibia,
Kisha wao kuambiwa, watakiwa kungojea,
Kingine kupakuliwa, mwaka ukisharejea,
Maneno tumeshashiba, tuna njaa ya vitendo.

Dhihaka wajionea, mingine kuingojea,
Leo leo vyatakiwa, uhaini kuwafaa,
Sio kuwangojea, maiti wameshakuwa,
Maneno tumeshashiba, tuna njaa ya vitendo.

Kitu hawatasikia, subira kutambuliwa,
Neno wanalingojea, kazi ikishatimia,
Miliki kuichukua, kufaidi manufaa,
Maneno tumeshashiba, tuna njaa ya vitendo.

Tena hawatangojea, kaya kujahadithiwa,
Wanataka kutumiwa, funguo za kufungua,
 Makasha yameshajaa, wenyewe wakachagua,
Maneno tumeshashiba, tuna njaa ya vitendo.

Vingine wataamua, vingine kuviondoa,
Usafi wakajitia, hadi mwaji kujimwagia,
Manukato wakatia, harufu kuziondoa,
Maneno tumeshashiba, tuna njaa ya vitendo.

Ubani kufukuzia, uoza ukafukiwa,
Pale wakijitambua, na dhamana kuitwaa,
Wawe wanajivunia, nchi yao imekuwa,
Maneno tumeshashiba, tuna njaa ya vitendo.




No comments: