Lakunjuliwa pazia, tuone yanayotokea,
Mwaka unakaribia, Januari kuingia,
Nangojea potezea,
jinsi zitakavyokuwa,
Pazia lafunguliwa, la sanaa na viroja !
Nazingojea sanaa, zitakavyonistua,
Akili zilizolemaa, wenda zikashtuliwa,
Hali yangu kurejea, uhakika nikajua,
Pazia lafunguliwa, la aibu na fedheha !
Pazia la madini gawa, na hisabu kupotea,
Akili kuzilalia, mfukoni kuzitia,
Na hongo kuinunua, uwezayo kununua,
Pazia lafunguliwa, la sanaa na viroja !
Pazia mafuta haya, na nani ayanunua,
Na mchezo kuchezewa, uwanja usiokuwa,
Bei ikapotezewa, na uchumi kuchafua,
Pazia lafunguliwa, la aibu na fedheha !
Pazia umeme njaa, njiani unaoishia,
Hamsini kutimia, robo haijafikia,
Visababu kwa gunia, haviachwi kutolewa,
Pazia lafunguliwa, la sanaa na viroja !
Pazia la maji mwaa, watu wasiyojionea,
Na ahadi zajifia, bila ugonjwa kujua,
Kilio kutosikia, ila mazishi yakawa,
Pazia lafunguliwa, la aibu na fedheha !
Pazia la ng'ombe waya, na vijosho vya kwogea,
Nasaba ikanukia, na ujanja wa kijuha,
Heri inakopepewa, hadi moto kuuzua,
Pazia lafunguliwa, la aibu na fedheha !
Pazia la Swizi gea, na vigia vya kutia,
Waliojikusanyia, na vilango kupitia,
Uchama ukawatoa, kama wanavyoutoa,
Pazia lafunguliwa, la sanaa na viroja !
Pazia la kufunikia, daktari kutegewa,
Kisa haki kulilia, ubaya akazuliwa,
Mwee, ninajichukia, kama nisiyezaliwa,
Pazia lafunguliwa, la aibu na fedheha !
Pazia la kufukia, wala si kufundishia,
Walimu walilolivaa, na kushindwa kuwafaa,
Vitumbua kugawiwa, vya kuokewa sheria,
Pazia lafunguliwa, la sanaa na viroja !
Batili yaendelea, na haramu yanadiwa,
Haki wameifungua, dhuluma waifungua,
Tarakimu kutimia, maajabu nangojea,
Pazia lafunguliwa, la aibu na fedheha !
No comments:
Post a Comment