WAOVU ukiachia, mabichi wanaaangua,
Wende kuvundukia, wewe usipopajua,
Juu kwa juu ikawa, bei wanapatania,
Amani yetu ni tunda, nani anatunza shamba ?
Miti msipoangalia, magugu hujiotea,
Ikawa shida kuzaa, mti unapohujumiwa,
Matatizo huzushiwa, hadi shamba kukimbia,
Amani yetu ni tunda, hivi mti twautunza ?
Na maji pasipokuwa, mti waweza sinyaa,
Mchwa wakafurahia, chakula chao kikawa,
Wakua ukidhania, kumbe wenda kujifia,
Amani yetu ni tunda, mti twastawishaje ?
La bibi linapokuwa, watu wakajichumia,
Hasara mtaingia, mwizi pasi kumjua,
Haki wamejigawia, nini utaambulia ?
Amani yetu ni tunda, shamba amiliki nani ?
Miti inapochakaa, mipya huwa yatakiwa,
Mbegu usipojaliwa, hutoweza jipandia,
Vya kale vikiendelea, huja kuvuna udhia,
Amani yetu ni tunda, mbegu twazipata wapi ?
Mti wataka mbolea, pia maji kumwagia,
Hasa katika dunia, mvua ilikopotea,
Bila hivyo kikawia, waweza jinyaukia,
Amani yetu ni tunda, mti twastawishaje ?
Jasho mwaweza kutoa, pasiwe cha kuambulia,
Sababu mia kutoa, kwanini mmefulia,
Ikawa kusingizia, tatizo kisichozua,
Amani yetu ni tunda, shamba amiliki nani ?
Sayansi inatakiwa, pia kwenda kutumia,
Sasa ni kunyunyizia, tone kwa kila hatua,
Kwayo mti ukakua, na maua kuchanua,
Amani yetu ni tunda, mbegu twazipata wapi ?
Maji katika dunia, sasa yanakopotea,
Mikakati yatakiwa, kidogo kutoshelea,
Watu wakaajabia, kuwa wasilodhania,
Amani yetu ni tunda, mti twastawishaje ?
Yajapo yakatokea, umiliki kuvamiwa,
Na wanaoyasimamia, wao pembeni kukaa,
Wakateza na sheria, kukunja na kukunjua,
Amani yetu ni tunda, shamba amiliki nani ?
Hasira huziibua, kwa wanaofatilia,
Kuwatuliza huvia, mishipa wakatanua,
Mhemuko ukikua, huja kuzuka balaa,
Amani yetu ni tunda, mbegu twazipata wapi ?
Mti ukijaugawa, pande moja kumwagia,
Ajabu haitakuwa, nusu kufa, nusu zaa,
Bali wote utavia, na mwisho kuteketea,
Amani yetu ni tunda, mti twastawishaje ?
Chanzo msipokijua, dalili mkaagua,
Huja kushtuliwa, maradhi yakizidia,
Hujivunga wakujua, kupata pa kupenyea,
Amani yetu ni tunda, shamba amiliki nani ?
Mbegu wakizifukua, wakaanza kujilia,
Pasiwe kurudishia, uhai kuendelea,
Watajazuka vichaa,
mapanga yakatembea,
Amani yetu ni tunda, mbegu twazipata wapi ?
Wanaoiba mbolea, na vipando kuvitwaa,
Vyao wakajifanyia, kwanza wanakimbilia,
Wengine wakafulia, huja wakaambuliwa,
Amani yetu ni tunda, mti twastawishaje ?
Juu waliokalia, budi macho kufungua,
Kwa sawa kuangalia, hali hasa wakajua,
Vingine ni kutania, na kuchezea dunia,
Amani yetu ni tunda, shamba amiliki nani ?
Nani anatuhadaa, mti tunaufatia,
Kisha tukajipandia,
huko tusikoruhusiwa,
Tunga linaning'inia, twataka kujichumia ?
Amani yetu ni tunda, shamba amiliki nani ?
Kila nikiangalia, haki na usawa bandia,
Mwivi namgundua, ndiye ananyemelea,
Macho tunawafumbia, vingine kusingizia,
Amani yetu ni tunda, shamba amiliki nani ?
No comments:
Post a Comment