Tuesday, December 11, 2012

Milizamu ya machozi


KILA nikikuwazia, au ndotoni ukawa,
Siaschi kujichekea, bila ya kujizuia,
Kisha chozi kuachia, mto wangu ukaloa,
Milizamu ya machozi,  ya kumbuko la furaha!

Thelathini yafikia, kama jana inakuwa,
Kwa ulivyoniangalia, kama mwana wa kuzaa,
Usingizini nikiwa, mashaka yalikimbia,
Milizamu ya machozi,  ya kumbuko la furaha!

Mikononi nilikuwa, sinalo la kukataa,
Moyo ulinifumua, na upya kuushonea,
Macho ukanifungua, kwa uzuri kugundua,
Milizamu ya machozi,  ya kumbuko la furaha!

Kicheko chako cha dawa, tiba kilinipatia,
Kwako sikuugulia, afya nilitunukiwa,
Mashaka sikuyajua, hadi ulipopotea,
Milizamu ya machozi,  ya kumbuko la furaha!

Kilio chako radhia, kilinipa ushujaa,
Bali sikujitambua, nini cha kushikilia,
Johari nikaachia, makapi kuyafatia,
Milizamu ya machozi,  ya kumbuko la furaha!

Muziki ulinipigia, kwangu ulio na hawa,
Midundo uliijua, kelele isiyokuwa,
Na nyingine nililia, machozi nikaachia,
Milizamu ya machozi,  ya kumbuko la furaha!

Na mingine nililia, machozi nikaachia,
Ukatwaa kitambaa, na uso kunifutia,
Kisha kunikumbatia, na busu kunigawia,
Milizamu ya machozi,  ya kumbuko la furaha!

Kupendwa sikujujua, hadi ulipotokea,
Mahaba nilisikia, kwako nikajionea,
Mizani nikitumia, uzito sijafikia,
Milizamu ya machozi,  ya kumbuko la furaha!

Nimebakia kulia, milizamu kuachia,
Furaha kunipotea, na upweke kunijaa,
Nipo kama nipo saa, hali navuta wasaa,
Milizamu ya machozi,  ya kumbuko la furaha!

No comments: