Saturday, December 29, 2012
Isije kuwa chooni
WENGINE siwaombei, ila nao kwepushiwa,
Nitakapokuwa hoi, maliwato kuzidiwa,
Ninatoa yangu rai, huko kutonitokea,
Isije kuwa chooni, mie pa kuondokea !
Shetani anakokaa, uchafu kufurahia,
Asikoona kinyaa, na najisi kujinywea,
Huko yasijetokea, pengine nikawahiwa,
Isije kuwa chooni, mie pa kuondokea !
Audhubillahi natia, shetani kutosogea,
Najilinda nikitambua, ulinzi nitaupewa,
Na palipo maridhia, mwisho wangu kufikia,
Isije kuwa chooni, mie pa kuondokea !
Waipendao dunia, thamani huko watia,
Yao wakayazuia, hata wengine kwingia,
Mimi ninalikataa, la umma nashuhudia,
Isije kuwa chooni, mie pa kuondokea !
Tunaowaigizia, hatua wamefikia,
Huko yanayatokea, macho twafunguliwa,
Sinemani yamejaa, ushetani umejaa,
Isije kuwa chooni, mie pa kuondokea !
Utajiri wa kung'aa, una tisho la kinyaa,
Thamani yawaishia, utu unawapotea,
Fedha inaabudiwa, na uungu inapewa,
Isije kuwa chooni, mie pa kuondokea !
Dhahabu yaabudiwa, hata roho ikatoa,
Dini sasa imekuwa, madhehebu ya bandia,
Majina wanayopewa, ya uongo na kuzua,
Isije kuwa chooni, mie pa kuondokea !
Shea washerehekea, ni ibada zimekuwa,
Watu kutiririkia, mitaani wapagawa,
Hesabu wakisikia, wawe wanashangilia,
Isije kuwa chooni, mie pa kuondokea !
Nukta zikifatia, kashfa budi kuzua,
Ujanja unazidia, ila mpya zazaliwa,
Yatosa teknolojia, kwa wale wasiojua,
Isije kuwa chooni, mie pa kuondokea !
Vizazi vinajiumbua, kufanyiana ubaya,
Kwa kupotea usawa, na uzito kulemea,
Haraka waliokuwa, za mkato kutumia,
Isije kuwa chooni, mie pa kuondokea !
Mia wakifurahia, elfu wao wanatwaa,
Kila mwenye kudokoa, yuko mwenye kuchimbua,
Adhaniaye apaa, kumbe hivi atembea ?
Isije kuwa chooni, mie pa kuondokea !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment