Deni hili hudaiwa, siku ya kuahidiwa,
Pasina kulitambua, kitanzi unajitia,
Kijana unatakiwa, muda wako kuujua,
Deni hili walijua, utakuja kudaiwa ?
Utakuja kuhojiwa, vipi uliutumia,
Ujana uliopewa, katika hii dunia,
Hesabu kuhesabiwa, kwa dakika na masaa,
Deni hili walijua, utakuja kudaiwa ?
Kipi ulijipangia, ya kwako kujifanyia,
Kisha ukaachia, ya Mola yaliyokuwa,
Na viumbe kuwafaa, waliowakikuttegemea,
Deni hili walijua, utakuja kudaiwa ?
Umri utatakiwa, na huo kuelezea,
Miaka uliyopewa, vipi uliitumia,
Uliifaa dunia, au ulijikusanyia?
Deni hili walijua, utakuja kudaiwa ?
Elimu huuliziwa, vipi uliitumia,
Baada kujipatia, nani iliyemfaa,
Ya dini na ya dunia, kiasi kuhesabiwa,
Deni hili walijua, utakuja kudaiwa ?
Kama uliizuia, kichwani ikabakia,
Haikuwa manufaa, kwa watu kusaidia,
Nakisi utaambiwa, makaa kuyanyakua,
Deni hili walijua, utakuja kudaiwa ?
Makaa kuyanyakua, ya moto yaliyokuwa,
Ugumuwe wa mwamba, jabali lililokuwa,
Huko ukaungulia, kwa kushindwa itumia,
Deni hili walijua, utakuja kudaiwa ?
Mali yatahukumiwa, mwenzetu uliyopewa,
Vipi uliyatumia, sio tu kwa kujifaa,
Bali ni kwa manufaa, wengine waliokuwa,
Deni hili walijua, utakuja kudaiwa ?
Waliojilim bikia, ili yote kutumia,
Katikati kuishia, mzigo huuchukua,
Kweli wakaambiwa, imewakusanya dunia,
Deni hili walijua, utakuja kudaiwa ?
Utadaiwa na afya, wewe uliyoipewa,
Vipi ulititumia, binadamu kuwafaa,
Na wanyama nao pia, haki wataililia,
Deni hili walijua, utakuja kudaiwa ?
Cheo waliopatiwa,milki kutumikia,
Swali hawatakimbia, vipi walikitumia,
Nani kilichomfaa, pasina kupendelea,
Deni hili walijua, utakuja kudaiwa ?
Wakubwa waliokuwa, nguo watajazivua,
Dini walioikataa, userikali ukawa,
Nani walimtumikia, Mola wakamzulia,
Deni hili walijua, utakuja kudaiwa ?
Marais nao pia, wanafiki walokuwa,
Swali kuwashtakia, dhamana kuichezea,
Uongo wanapozua, watu wakasingizia,
Deni hili walijua, utakuja kudaiwa ?
Waliofata umbeya, haki wakapuuzia,
Yote kuzungumziwa, na mizani kupimia,
Kisha yakaamulia, kule kunakowafaa,
Deni hili walijua, utakuja kudaiwa ?
Michache imebakia, kutubu wanatakiwa,
Kaburi lajifungua, dhuluma kuziondoa,
Siku hiyo yaingia, wapaswa kuingojea,
Deni hili walijua, utakuja kudaiwa ?
Wabunge wa kutumia, fursa wataipewa,
Wao wakauliziwa, nani waliyemfaa,
Kama ndio wajilia, hukumu wajichongea,
Deni hili walijua, utakuja kudaiwa ?
Na walionunuliwa, bei watauliziwa,
Kiasi walopewa, watu wakajiuzia,
Na nchi kujinadia, fedha wakaichukua,
Deni hili walijua, utakuja kudaiwa ?
Viongozi watalia, dhuluma wakiijua,
Vipi watailipia, saa kuwageukia,
Na kilichowazuzua, muda hakikuchukua,
Deni hili walijua, utakuja kudaiwa ?
Maumbo waliyopewa, mazuri yaliyokuwa,
Nao watauliziwa, vipi waliyatumia,
Kama heri ilikuwa, faida kwao ikawa,
Deni hili walijua, utakuja kudaiwa ?
Uwezo waliopewa, la kwao litatakiwa,
Vipi waliutumia, katika hii dunia,
Kama waliuchezea, kilio wataangua,
Deni hili walijua, utakuja kudaiwa ?
Ujanja waliojaliwa, nao watauliziwa,
Kama watu ulifaa, au uliwaibia,
Kisha wakasiginiwa, motoni chini kukaa,
Deni hili walijua, utakuja kudaiwa ?
Akili waliopewa, nao watauliziwa,
Kwa mema walitumia, au ubaya kuzua,
Kisha wakahukumiwa, haki yao wakapewa,
Deni hili walijua, utakuja kudaiwa ?
No comments:
Post a Comment