Monday, December 24, 2012

C H A M A ?

 
USHABIKI wa kijinga, zama zake zaishia,
Watu sasa wanachanga, yenye hoja kuchengia,
Si rahisi kuwavunga, njia wakazifungua,
kodi yajenga taifa, toka lini kiwe chama ?
Kodi yajenga taifa, toka lini kiwe chama ?
 
Uongo wakiizua, ukweli watajibiwa,
Hakuna asiyejua, kodi yajenga dunia,
Wao wakituambia, vingine hatutajua,
Kodi yajenga taifa, toka lini kiwe chama ?
 
Yeyote anayekuwa, dola ameichukua,
Hukusanya kikajaa, kisha akakitumia,
Kula haiwi ridhaa, ila watu kuwafaa,
Kodi yajenga taifa, toka lini kiwe chama ?
 
Wao inaelekea, huanza kwa kujilia,
Kisha wakavigawa, kwa ndugu pia jamaa,
Kidogo kinachobakia, ndio wakatuhadaa,
Kodi yajenga taifa, toka lini kiwe chama ?
 
Vikubwa vingelikuwa, vyema ingelitumia,
Kodi tuliyoitoa, wala ndogo haikuwa,
Ujanja wametumia, bianfsi kuwafaa,
Kodi yajenga taifa, toka lini kiwe chama ?
 
Kwa uongo kuutia, ndio watu wachukia,
Ukweli mkiutoa, watu watawaelewa,
Mlavyo mmejaliwa,nafasi mliyokaa,
Kodi yajenga taifa, toka lini kiwe chama ?
 
Ila si kutuambia, wengine watafulia,
Kazi hawataijua,ila mliojaliwa,
Ndio tu mnaelewa, hazina kusimamia,
Kodi yajenga taifa, toka lini kiwe chama ?
 
Kama hivyo kungekuwa, vipi nako kwaibiwa,
Milango mmefungua, au chama kujifaa,
Mbona mwagugumia, ukweli hatujajua ?
Kodi yajenga taifa, toka lini kiwe chama ?
 
Uongozi si sanaa, ujuzi unatakiwa,
Na kila mwenye kujua, siasa alielewa,
Vingine haitakuwa, ila kwa wanaoelwa,
Kodi yajenga taifa, toka lini kiwe chama ?
 
Ila kwa wanaoelwa,  watakao kuimbiwa,
Mapambo wakapambiwa, matapishi yamejaa,
Kinyqa kisipokuwa, maajabu hutokea,
Kodi yajenga taifa, toka lini kiwe chama ?
 
Kodi dereva ikiwa, nchi inatengamaa,
Udhibiti usopwaya, malengo yakatimia,
Watu wakajisema, nchi yenyewe yakuwa,
Kodi yajenga taifa, toka lini kiwe chama ?
 
Kodi ikishachezewa, haliwi hata la kuwa,
Kila kitu kitapwaya, na chuki zikaanzia,
Wenyewe kujiibia, hayo huwa yatokea,
Kodi yajenga taifa, toka lini kiwe chama ?
 
Uswizi zinazokaa, watu hazijawafaa,
Huenda wakajifia, kisha bure kupotea,
Na wana kuwa vichaa, zikashindwa kuwalea,
Kodi yajenga taifa, toka lini kiwe chama ?
 
Batili ikitumiwa, mtenzi anaumia,
Awali hakuyajua, ukubwani hutokea,
Macho akifungulia, roho akaagulia,
Kodi yajenga taifa, toka lini kiwe chama ?
 
Haki ya mtu kuliwa, hilo halijaruhusiwa,
Kuna siku huwadia, deni kwenda kulipiwa,
Kama baba haikuwa, wana wake itakuwa,
Kodi yajenga taifa, toka lini kiwe chama ?
 
Tamaa waliojaa, kidogo wakipokea,
Kikubwa hukiachia, kikaenda kupotea,
Yao wakaangalia, si yetu kutulindia,
Kodi yajenga taifa, toka lini kiwe chama ?
 
Kumbe kinachotokea, ni kama kupotezea,
Wakuu wakishapewa, ni ruhusa kupotea,
Udhibiti twafulia, bado tunashangilia ?
Kodi yajenga taifa, toka lini kiwe chama ?
 
Hazina inachopokea, hivi nusu chafikia,
Mwakyembe akitua, mbona kingi chavuliwa ?
Nini kinachotokea, mbona hamjatwambia,
Kodi yajenga taifa, toka lini kiwe chama ?
 
Hivi kadi ya Slaa, ni mazito kuliko haya,
Chama mnatuhumiwa, mashamba ya bibi kunywea,
Au hamjasikia, huko mnakopitia ?
Kodi yajenga taifa, toka lini kiwe chama ?
 
Itajengwa Tanzania, fedha zisipopotea,
Nyie mnaziachia, watu waenda chezea,
Mtu milioni mia, kwa siku moya azoa ?
Kodi yajenga taifa, toka lini kiwe chama ?
 
Marudufu yakitua, kisha vyema kutumiwa,
Itafufuka Tanzania, na kisha kuanza kupaa,
Hapo stahi itakuwa, sasa kuanza sifiwa,
Kodi yajenga taifa, toka lini kiwe chama ?
 
Kujipanga yatakiwa, tena haraka ikawa,
Kizidicho kuingia, wachache kutojilia,
Kumbe tulichojaliwa, wote chaweza tufaa ?
Kodi yajenga taifa, toka lini kiwe chama ?
 

No comments: