Monday, December 24, 2012
Mizizi nishaing'oa
YA UDIKTETA 'meng'oa, kidogo tu yabakia,
Shamba mikikazania, lote safi litakuwa,
Ila tu kama ikiwa, nanyi mtanunuliwa,
Mizizi nishaing'oa, uchafu kafagieni !
Kazi nilijitolea, mwenyewe kujifanyia,
Kizazi niweze faa, wasiukute udhia,
Magugu kushughulikia, taabu yatakayozua,
Mizizi nishaing'oa, uchafu kafagieni !
Enendeni mnajua, kupanda tu yabakia,
Mkiamua mvua, mnaweza kungojea,
Ila nimewachimbia, kisima cha kutumia,
Mizizi nishaing'oa, uchafu kafagieni !
Mwaweza kujilimia, pasina hiyo mvua,
Maji mkiyapakua, mnaweza kumwagiwa,
Kilimo kuendelea, bila ya kuachilia,
Mizizi nishaing'oa, uchafu kafagieni !
Haki mkiililia, uhuru sasa mkawa,
Ya uchumi kuamua, wenyewe kujifanyia,
Bila yakuwangojea, wajanja wa huko Daa,
Mizizi nishaing'oa, uchafu kafagieni !
Kuna nchi nawambia, ni ndogo kuliko mkoa,
Duniani zimejaa, uchumi wao wa paa,
Hil yetu ni dunia, kwa ukubwa yazidia,
Mizizi nishaing'oa, uchafu kafagieni !
Wamoja twaweza kuwa, ila kwa kujitegemea,
Katikati tukakaa, ya pamoja kuyajua,
Ya uchumi si radhia, wasokwepo kuachiwa,
Mizizi nishaing'oa, uchafu kafagieni !
Haya yataka hatua, kila siku kuchukua,
Mashine tukatumia, ngamizi zilizokuwa,
Ikawa twafatilia, kwa usiku na mchana,
Mizizi nishaing'oa, uchafu kafagieni !
Haitulii dunia, na kulala ni balaa,
Sisi tukijilalia, tutakuja tawaliwa,
Miji inatakiwa, usingizi kukimbia,
Mizizi nishaing'oa, uchafu kafagieni !
Watu hujilalia, si kwa usiku kwingia,
Ila wakijichokea, nguvu zipate rejea,
Kisha wakendelea, mapinduzi kuyazua,
Mizizi nishaing'oa, uchafu kafagieni !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment