Saturday, December 29, 2012
Kaolewe na benki
Naona yastahiki, benki wewe kukuoa,
Kwani wazidi hamaki, fedha kuipigania,
Kumbe wewe mamluki, na ndoana yako ndoa,
Kaolewe na benki, kiumbe usotosheka !
Senti waona ni haki, sikuzote kupatiwa,
Hali hazitabiriki, siku katika dunia,
Yaliyokuwa afiki, nayo sasa yakataa,
Kaolewe na benki, kiumbe usotosheka !
Somo haufundishiki, wataka jana kwendelea,
Hilo haiyumkiniki, haliwezi kutokea,
Kama haubadiliki, kituo ninakijua,
Kaolewe na benki, kiumbe usotosheka !
Dunia ni ushiriki, kazi mkajipangia,
Na matumizi ya dhiki, wote mkayagundua,
Ili mjenge lukuki, njia zenye kuwafaa,
Kaolewe na benki, kiumbe usotosheka !
Tusiifanye hamaki, tukaja kujichongea,
Dunia haiaminiki, upendo wao wa riha,
Fakiri hathaminiki, wote watatukimbia,
Kaolewe na benki, kiumbe usotosheka !
Tunafaa kudiriki, tuanze kuzua mapya,
Tukimbie unafiki, kwa kesho kuangalia,
Nini lenye stahiki, linaweza kutufaa,
Kaolewe na benki, kiumbe usotosheka !
Nikiwa ni mabruki, haya tutajivukia,
Mengi tukastahiki, leo tusiyoyajua,
Ila huko hatufiki, kama leo twachezea,
Kaolewe na benki, kiumbe usotosheka !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment