Saturday, December 29, 2012

Kweli mwalimu dunia



Ukweli akikwambia, kujali unatakiwa,
Somo ameliandaa, na dunia aijua,
Wewe ukalikataa, mwenyewe utaumia,
Kweli mwalimu dunia, kazi yake anajua!

Uongo akikwambia, fupi huwa yake njia,
Wewe ukauchagua, maisha kukusaidia,
Hatua itafikia, ukweli ukatambua,
Kweli mwalimu dunia, kazi yake anajua!

Wizi akihofia, huja ukakuumbua,
Wewe ukajichekea, na kazi kwendelea,
Siku ya kushtukiwa, moto unaweza tiwa,
Kweli mwalimu dunia, kazi yake anajua!

Haki akikuambia, vibaya kujiuzia,
Wewe ukamtania, na lako kuendelea,
Huja siku kweli kuwa, haya ukajionea,
Kweli mwalimu dunia, kazi yaek anajua!

Zinaaa akihofia, pabaya hukuchukua,
Wewe ukamnunia, na batili kuingia,
Yanapokujatokea, mbali nawe atakuwa,
Kweli mwalimu dunia, kazi yake anajua!

Tamaa akikumbia, hukuingiza pabaya,
Wewe ukajichekea, na kuilea tabia,
Itakuja kuumbua, naye kajiondokea,
Kweli mwalimu dunia, kazi yake anajua!
Uroho akikuambia, waweza kugeukia,
Wewe usiposikia, yanakujakutokea,
Kisha ukajililia, ujinga uliokuwa,
Kweli mwalimu dunia, kazi yake anajua!

Uchu akikuambia, athari kuangamia,
Wewe ukapuuzia, na yako kuendelea,
Siku yakijajizoa, na wewe hutojijua,
Kweli mwalimu dunia, kazi yake anajua!

Watu akikuambia, kuheshimiwa wafaa,
Na thamani kuijua, masihani kiingia,
Wewe ukalikataa, utakuja lijutia,
Kweli mwalimu dunia, kazi yake anajua!

Wazazi wakifulia, itakufunza dunia,
Bila fimbo kuchukua, yakabidi kuingia,
Tena laivu yakawa, mwenyewe wajionea,
Kweli mwalimu dunia, kazi yake anajua!'

Alimu namuachia, njia anayeijua,
Kizazi kuangalia, kisiwe kinapotea,
Njia usiyoijua, haifai kuingia,
Kweli mwalimu dunia, kazi yake anajua!

No comments: