Friday, November 2, 2012

Chanzo usipokijua





MARADHI ukiugua, vyema kiini kujua,

kama usipokijua, bure unajisumba,

Weza ukasingizia, ugonjwa usiougua,

Chanzo usipokijua, mtabaki hangaika !



Weza ukasingizia, ugonjwa usiougua,

Dawa ukazitumia, sahihi zisizokuwa,

Rangi kuwa kahawia, au zambarau ukawa,

Chanzo usipokijua, mtabaki hangaika !



Mambo ya kuyasikia, bila ya kujionea,

Ni umbeya kuulea, Daudi aliambiwa,

Lawama zikiingia, ushahidi watakiwa,

Chanzo usipokijua, mtabaki hangaika !



Ushahidi watakiwa. upande mshtakiwa,

Na yeye kuelezea, jinsi ilivyotokea,

Mmoja ukiiusikia, haki inahujumiwa,

Chanzo usipokijua, mtabaki hangaika !



Mashahidi watakiwa, huru wanaotambuliwa,

Pande wasiolalia, na cha mbele kuchukua,

Adili waliojaliwa, na utu wanaojua,

Chanzo usipokijua, mtabaki hangaika !



Sio wa kuwanunua, mfukoni walotiwa,

Imani mfu ikawa, na haya inshapotea,

Wasafi wanatakiwa, kote wakaaminiwa,

Chanzo usipokijua, mtabaki hangaika !



Chanzo watu wanazua, kingine kikaja kuwa,

Uongo wenye hadaa, ya matumbo yenye njaa,

Wapikwa na kutumiwa, waso aibu wapewa,

Chanzo usipokijua, mtabaki hangaika !



Chanzo ukweli chajua, halali kinapokuwa,

Si dalili kudhania, ndio kiini kimekua,

Kosa utaliingia, uwe wa kulaumiwa,

Chanzo usipokijua, mtabaki hangaika !



Chanzo kama mshumaa, au hata bora taa,

Nuru huwa kinatoa, palepale ukajua,

Vinginevyo ikiwa, unaicheza nazaa,

Chanzo usipokijua, mtabaki hangaika !

No comments: