Sunday, November 18, 2012

KIONGOZI WA UKWELI


ZAMA za kujilimbia, zafaa wasiojijua,

Karibu wa kuangalia, wasiojua dunia,

Kitu wasiosikia, ila kujaliwa raha,

Kiongozi wa ukweli, hatojishibisha kwanza:

Huwashibisha raia.



Wa kweli anayekua, kula atajachelewa,

Mbele hatakimbilia, na sinia kachukua,

Ila nyuma atakaa, kikombe kakumbatia,

Kiongozi wa ukweli, hatojishibisha kwanza:

Huwashibisha raia.



Hatopenda kutumia, kwa kuwa nchi yatoa,

Mbali hatakimbilia, karibu kuangalia,

Watu hatosaidia, ila uwezo kuvua,

Kiongozi wa ukweli, hatojishibisha kwanza:

Huwashibisha raia.



Si wa kusimulia, ya watu kuyasikia,

Huchuja kwa hilo kawa, na vichujio kadhaa,

Yote akaangalia, kwa pembe zenye kuzua,

Kiongozi wa ukweli, hatojishibisha kwanza:

Huwashibisha raia.





Vichache huvichagua, vya haraka kuchanua,

Mkazo akatilia, kazi viweze fanziwa,

Hivyo vikishakua, vingi sana huvizaa,

Kiongozi wa ukweli, hatojishibisha kwanza:

Huwashibisha raia.



Watu wake huwajua, sio kuwasingizia,

Ugomvi wetu ni njaa, malau pia balaa,

Na dharau za mkaa, mweupe zisizofdaa,

Kiongozi wa ukweli, hatojishibisha kwanza:

Huwashibisha raia.



Kama vile motokaa, gia zake hutambua,

Ya kwanza ikishaingia, zingine zinafatia,

Ndivyo ilivyo dunia, yapo ya kutangulia,

Kiongozi wa ukweli, hatojishibisha kwanza:

Huwashibisha raia.



Halisi ninatambua, lipo hili lenye njaa,

Bei ukizitanzua, maisha nafuu huwa,

Wala si kujisifia, milioni wafulia,

Kiongozi wa ukweli, hatojishibisha kwanza:

Huwashibisha raia.



No comments: