Wednesday, November 14, 2012
Mwonewa akigeuka
Akija kuwa mwonea, kwa aliyekionewa,
Kisasi akakitia, mtima kuutumbua,
Huwa fukwe zaambaa, baharini kuingia,
Mwonewa akigeuka, akaja kuwa mwonea !
Maji ardhi huvaa, pwani yote kutembea,
Mradi ukauzua, wa damu kwenda jitoa,
Ya siri usiyojua, dhahiri yakatokea,
Mwonewa akigeuka, akaja kuwa mwonea !
Mwili hawajaujua, ni mmoja ulokuwa,
Ule ukiuonea, wako nao waumia,
Na hili halijakuwa, ila kwa waliojaliwa,
Mwonewa akigeuka, akaja kuwa mwonea !
Viumbe wote wamoya, vingine haijawa,
Kizazi kilozaliwa, asili twaitambua,
Vipi jino kujitoa, uchungu kutosikia ?
Mwonewa akigeuka, akaja kuwa mwonea !
Wewe unalofurahia, mwenzi alihitajia,
Majivuno ni udhia, tena mkubwa balaa,
Vya msingi vyatakiwa, kila mtu kuambua,
Mwonewa akigeuka, akaja kuwa mwonea !
Vitu wanaoringia, umoja wanauua,
Ndipo huja kuzaliwa, tamaa waliojaa,
Elfu kuiridhia, hata mtu kumuua,
Mwonewa akigeuka, akaja kuwa mwonea !
Roho zao huziua, utu wakaufikia,
Vigumu kutambua, na heri yasiyokuwa,
Ubayani kubakia, hadi roho kutolewa,
Mwonewa akigeuka, akaja kuwa mwonea !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment