MBEGU wamezitupia, katika mawe kuota,
Miye nimeangalia, na ugumba kuusuta,
Kama vile ni ruia, bado ningali naota,
Mizizi katika mawe, mmea hauachi kufa !
Yao walikimbilia, na wakanipita puta,
Nyuma hawakuangalia, ya mbele wakiyafata,
Chini hawakuangalia, niendapo waokota,
Mizizi katika mawe, mmea hauachi kufa !
Wafata historia, inayozidi wasuta,
Yamebakia mazoea, umeanguka ukuta,
Nao wanaegemea, huku wangali watweta,
Mizizi katika mawe, mmea hauachi kufa !
Mambo wameyapangua, wabaki cheza karata,
Kesho inawachachia, wanatifua matuta,
Vyanzo wanakovijua, sasa ufuta wateta,
Mizizi katika mawe, mmea hauachi kufa !
Hali ninaihofia, inanukia matata,
Mwanzo itapaanzia, kuongezeka ukata,
Watu wakajinunua, acha wa kununuliwa,
Mizizi katika mawe, mmea hauachi kufa !
Mbata wataziangua, na miembe kupukuta,
Na mbichi zilizokuwa, moto ziende kuota,
Hali ikishafikia, watalitwanga pepeta,
Mizizi katika mawe, mmea hauachi kufa !
Mizizi mkitifua, mtake tena kuota,
Ardhi huikataa, vya chini vikatokota,
Chinichini kutambaa, juu yashindwe kupita,
Mizizi katika mawe, mmea hauachi kufa !
Mkikota mimea, na watu kuwaokota,
Lipi la kujipandia, hadi hadhi kuipata,
Miaka itaamua, yaishe ya kumetameta,
Mizizi katika mawe, mmea hauachi kufa !
Mti hauwezi kua, wala tunda kulipata,
Mizizi ikijifia, huwa vigumu kuota,
Taratibu hujifia,ikabakia kutweta,
Mizizi katika mawe, mmea hauachi kufa !
Mliyoyakimbilia, ikawa sasa kunyata,
Na kilichowazuzua, kikabakia kiota,
Mahame yakabakia, na njia zilizotota,
Mizizi katika mawe, mmea hauachi kufa !
Sunday, November 18, 2012
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment