Thursday, November 8, 2012
Rushwa kwisha haiwezi
WAKUU wakiamua, chamani kutoridhiwa,
Tutaipiga hatua, usafi ukarejea,
Haya tukivumilia, naona twenda pabaya,
Rushwa kwisha haiwezi, ila yaweza pungua !
Uchina yanatokea, na watu wanauawa,
Chama kimekazania, chamani kutoachiwa,
Ole wako 'kigunduliwa, risasi ni yako dawa,
Rushwa kwisha haiwezi, ila yaweza pungua !
Chama chajifaragua, serikali kutokuwa,
Mangimeza kwangaliwa, wasije wakapotea,
Udhibiti watimia, kila siku wafichua,
Rushwa kwisha haiwezi, ila yaweza pungua !
Usafi hadhi hutia, chama kutodharauliwa,
Haya ukiyakataa, juu sana kitakuwa,
Vinginevyo 'kiachiwa, kusambaratika kwawa,
Rushwa kwisha haiwezi, ila yaweza pungua !
Yafaa kujiangalia, binafsi tulokuwa,
Mzigo tukishakuwa, mapema kujichomoa,
Ni vizuri kujifia, ili chama kwendelea,
Rushwa kwisha haiwezi, ila yaweza pungua !
Sasa tuking'ang'ania, riziki haitakuwa,
Makubwa nayahofia, chama kuja kusumbua,
Si safi hali ya hewa, kwa mashine twapumua,
Rushwa kwisha haiwezi, ila yaweza pungua !
Ukiongeza na njaa, nchi inayosumbua,
Wahasirika jamaa, baya watavumiia?
Mikono wakinyanyua, nani atayeumia?
Rushwa kwisha haiwezi, ila yaweza pungua !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment