Sunday, November 18, 2012
Halali na haramu
YA halali na haramu, viumbe mmeumbiwa,
Mkapewa na fahamu, tofauti kuijua,
Kafiri na Islamu, wote hili walijua,
Mwatakiwa kuyajua, ya halali na haramu !
Kukumbusha yangu zamu, wote mnaofatia,
Nisiwe wa kudhulumu, kuwa hili sikwambia,
Nalijua, situhumu, ukweli nauridhia,
Mwatakiwa kuyajua, ya halali na haramu !
Kumbukeni Jahanamu, muweze kuikimbia,
Mkijitia muhimu, na hili kutohofia,
Maisha ni madhulumu, huruma hayajapewa,
Mwatakiwa kuyajua, ya halali na haramu !
Yakuuliza kalamu, miaka ulivyotumia,
Kama una elimu, hesabu utadaiwa,
Na ujana wa hanjamu, kizaazaa huzua,
Mwatakiwa kuyajua, ya halali na haramu !
Mali ukitakadamu, nayo itauliziwa,
Na cheo ukikihimu, kuna deni wadaiwa,
Mchungi huna utamu, hadi hesabu kuijua,
Mwatakiwa kuyajua, ya halali na haramu !
Niepushe na haramu, halali kunijalia,
Nakuomba Mukadamu, dua yangu kusikia,
Sijaliwi ufahamu, ila unaonijalia,
Mwatakiwa kuyajua, ya halali na haramu !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment