Thursday, November 8, 2012
Refa rafu akianza
JARIBU kufikiria, mechi inaendelea,
Kisha refa kaamua, yeye ndiye kuanzia,
Pande zote kabutua, na viatu kuwatia,
Refa rafu akianza, uwanja vipi 'takuwa ?
Urefa akaamua, pekee yeye akawa,
Wasaidizi kapewa, yeye amewakataa,
Lao ameligomea, hataki kulikisikia,
Refa rafu akianza, uwanja vipi 'takuwa ?
Watu wanamuhofia, kaingia ukichaa,
Au ameishapagawa, mke amemkimbia?
Au nzaiko imekoa, mwenyewe kumuingia?
Refa rafu akianza, uwanja vipi 'takuwa ?
Kadi ovyo anatoa, wachezaji wapungua,
Na sasa wamebakia, wachache wasotimia,
Mashabiki wazomea, hivi sasa ni udhia,
Refa rafu akianza, uwanja vipi 'takuwa ?
Mechi yataka nasaha, na vingi kuvumilia,
Haraka ukiamua, utamu wote hupaa,
Shubiti ikabakia, na mawe kukufatia,
Refa rafu akianza, uwanja vipi 'takuwa ?
Misongo isipoachiwa, mafuu huambulia,
Wengi kuchanganyikiwa, mengine wakaamua,
Kimya ukikisikia, mshindo utatokea,
Refa rafu akianza, uwanja vipi 'takuwa ?
Uwanja wakiumbia, wapi utawaonea,
Na vipi utalijua, watakalojisukia,
Mke gunia huvaa, mme gauni kuvaa,
Refa rafu akianza, uwanja vipi 'takuwa ?
Cheichei naitoa, kwa ndgu nao jamaa,
Mwana ameshambiwa, kuzika imebakia,
Nguu mlima haijawa, safari sasa upya,
Refa rafu akianza, uwanja vipi 'takuwa ?
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment