Sunday, November 18, 2012

Wajumbe tena hatuna



Wajumbe tumepoteza, watumwa wanabakia,

Viumbe wakujiuza, mfukoni wametiwa,

Kwa sasa ni kama viza, yai lisilotufaa,

Sasa tunao watumwa, wajumbe tena h atuna !



Wajumbe wachiuza, uwakilishi kuua,

Nchi tunaipoteza, kama nguo kuivua,

Uchi kujitembeza, ikatucheka dunia,

Sasa tunao watumwa, wajumbe tena h atuna !



Kazi wanaoongoza, wanasiasa Tanzania,

Vyama bila kutangaza, hakuna asiyejua,

Ujumbe sasa kujiuza, na kura ikanunuliwa,

Sasa tunao watumwa, wajumbe tena hatuna !



Dini ilishapoteza, udini wakataliwa,

Ila roho wanauza, kuizuia dunia,

Wadhania waongoza, kumbe wanaangamia,

Sasa tunao watumwa, wajumbe tena h atuna !



Ni samaki wameoza, kwenye tenga walojaa,

Vikundi wanavyokuza, vya njaa kujigangia,

Fedha wanatanguliza, Nyerere alohofia,

Sasa tunao watumwa, wajumbe tena h atuna !



Siasa waendeleza, ufukara kuulea,

Wao wanavyoangaza, utumwa wasaidia,

Njaa watu ikiliza,mkubwa unabakia,

Sasa tunao watumwa, wajumbe tena h atuna !



Hawataki kuongoza, umaskini kutoa,

Wajua haya wakifanza, uhutu twajipatia,

Na kuringa tutaanza, kurani kuwakataa,

Sasa tunao watumwa, wajumbe tena h atuna !



Hivyo wanang'ang'aniza, ufukara kubakia,

Kwao ngao wanatunza, ukubwa kutopotea,

Ajabu ya muujiza, na ibra ya dunia,

Sasa tunao watumwa, wajumbe tena h atuna !



Heshima waipoteza, wao wanajisifia,

Hata watoto wajuza, ni kicheko imekuwa,

Baba na mama kutunzwa, ardhi wakaiachia ?

Sasa tunao watumwa, wajumbe tena h atuna !



Na tena wanachotunzwa, ni chache zao rupia,

Thamani zimepoteza, kitu hazitosaida,

Laiti wangejitunza, tajiri wangelikuwa,

Sasa tunao watumwa, wajumbe tena h atuna !



Mazoe kumbe kuoza, wachache wanaojua,

Kila unapoangaza, hali ukakubalia,

Kumbe juu ungeweza, aliye akuzuia,

Sasa tunao watumwa, wajumbe tena h atuna !



Akili wanakuteza, na mitego kukwekea,

Wajua hujui tunza, wala kujitafutia,

Hivyo wanakulemaza, waweze kukutumia,

Sasa tunao watumwa, wajumbe tena h atuna !









No comments: