Sunday, November 18, 2012

Ni mwepesi wa kupanga

Barri ni mwenye kujua, hata tusiyoyajua,

Na anapotangulia, wasiwasi hututoa,

Tusijifanye twajua, chicha tukaambulia,

Ni mwepesi wa kupanga, huwezi shindana naye !



Asili tunaijua, twakubali nunuliwa,

Mfukoni tukatiwa, ya wengine kuriddhia,

Hali fika tunajua, twaweza jitegemea ?

Ni mwepesi wa kupanga, huwezi shindana naye !



Yetu tukijipangia, mbele budi kusogea,

Kuna ndugu wangojea, mkono kutupatia,

Vigumu haitakuwa, dini yetu waijua,

Ni mwepesi wa kupanga, huwezi shindana naye !



Hadithi zasimuliwa, bara yaliyotokea,

Jerumani kashupaa, udini kuutambua,

Hisabu wakachafua, ili kwenda waridhia,

Ni mwepesi wa kupanga, huwezi shindana naye !



Ndio kisa kukataa, ubaya lisilokuwa,

Mbona leo twasikia, Marikani waridhia,

Kura walipojipigia, dini siri haikuwa,

Ni mwepesi wa kupanga, huwezi shindana naye !



Ujanja wakitumia, pabaya wanatutia,

Wajifanyao kujua, ikawacheza dunia,

Aibu yawaingia, hadi nje wahofia ?

Ni mwepesi wa kupanga, huwezi shindana naye !



Data kaziye kuzaa, yote nje kuanikwa,

Vingine haijakuwa, uongo unapotia,

Kazi hazitowafaa, hubakia kuchezewa,

Ni mwepesi wa kupanga, huwezi shindana naye !



Takwimu zakuchambua, kisha zikabanguliwa,

Zinakuwa na udhia, kupikwa huja kataa,

Chunguni kinachotiwa, kibichi kikabakia,

Ni mwepesi wa kupanga, huwezi shindana naye !



No comments: