Nani kalifikiria, na chama kukigawia,
Iweje sera ikawa, chama inazinunua,
Na sote twatarajia,, kwa yake tukajaliwa,
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Labda rushwa kutoa, hiyo ya kwao twajua,
Ufukara kuzidia, ndipo hapa tumekaa,
Na upofu kujitia, kitu halijasaidia,
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Kwa uziwi kusifiwa, haya tungeishajua,
Ya msingi yamejaa, kufanza tunatakiwa,
Hapo tukishafikia, sera twaweza ibua,
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Nani amekuambia, kwenye hii Tanzania,
Kuna watu wakataa, kilimo kutuhudumia,
Na vyama tumevizua, chakula kutotumia ?
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Nani amekuambiwa, kunao Watanzania,
Gizani waazimia, sikuzote watakaa,
Vijinga wakatumia, mwangaza kujipatia,
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Na eti wa kuwatoa, budi mchama akawa ?
Kama mtu hujifia, hicho cha kutegemewa ?
Na mumiani kikiwa, ndio hofu kinatia,
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Nani amekuambia, chama fedha kimejaa,
Wapi kinajipatia, kama si hazina pia,
Kingi wakakumbatia, kidogo wakaachia,
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Serikali kuzifua, lazima inatakiwa,
Leo moja ukavaa, kesho nyingine kutwaa,
Nguo moja kitumia, fukara utadhaniwa,
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Serikali ni kuvaa, na kisha ukaivua,
Unapoing'ang'ania, inazidi kuchakaa,
Uzuri haitakuwa, ikianza kufubaa,
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Jana kijani kutia, leo bluu watumia,
Rangi nyingi zimejaa, moja tu unachagua,
Kuna zingine balaa, bahati hukukimbia,
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Nani amekuambia, njia wanazikimbia,
Wazihofu Tanzania, kuwaletea mabaa,
Maporini wapitia, salama kujisikia?
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Sera ni kama bidhaa, vitu hivyo hutumiwa,
Vitu vinapomfaa, kila mtu hutumia,
Ila kama vya rushuwa, muumini hukataa,
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Sera kama vile hewa, kila mtu hupumua,
Mazuri kuyachagua, binadamu ni tabia,
Hawezi akaparamia, baya yeye kuchagua,
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Nani amekuambia, elimu haitatufaa,
Hivyo wajinga wang'aa, elimu kuitania,
Na mikopo kuzuia, wenetu kutowafaa?
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Nani amekuambia, ataka lima kinjaa,
Pamba akijivunia, soko kutotengenea,
Akasikiza umbeya, na hadithi kupigiwa ?
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Nani amekuambia, afya ni kitu balaa,
Huduma bure kutoa, watu wengi wahofia,
Ila ujira wa njaa, ukawa wapalilia,
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Ila ujira wa njaa, ukawa wapalilia,
Dau wakalizindua, sasa milioni kuwa,
Senti zikishapungua, huondoka wako dia,
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Nani amekuambia, eti nyumba twakataa,
Manyata twakumbatia, na porini kutulia,
Mjini twakuhofia, hatutaki kwendelea,
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Kama sio yenu nia, fahari kujionea,
Neema kujisikia, nyie mliojaliwa,
Vyote kuwatiririkia, wote mliobarikiwa,
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Siri wameigundua, mwahofu kukataliwa,
Binti ukimjengea, aweza nje kukutoa,
Mwingine kukubaliwa, na kitu asiyekuwa,
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Kwenu ni Watanzania, wanajua kuchagua,
Nyumba wakijipatia, wengine watachangua,
Uhuru kujipatia,, hamwezikuwaswagia,
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Nani amekuambia, wageni ndio wafaa,
Kukopa tukijazia, mabenkini zikajaa,
Ila akiwa mzawa, shuruti anaekewa ?
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Nani amekuambia, hatutakiwi Ulaya,
Pasi mkazizuia, wenyeji kujipatia,
Ila wa Somalia, raia wao wakawa ?
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Nani amekuambia, juujuu ukijua,
Mweledi umeshakua, bila ya kuyachunua,
Ng'ombe wayo huuziwa,mjini ukaingia,
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Nani amekuambia, hisa tumeshazikataa,
Ila palipo udhia, utani pia mzaha,
Oksijeni kwishiwa, bado najiulizia ?
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Nani amekuambia, madini yamilikiwa,
Na wachache walokuwa, matofali wakapewa,
Nani anayetumia, ujira akishapewa ?
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Langu ninamalizia, kwa uchama kukataa,
Mengi yanayotakiwa, hayo ya wote yakawa,
Programu kuridhia, nchini kufumuliwa,
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Serikali ya pamoya, akili iliyojaa,
Hiyo nitafurahia, na sio ya kutumiwa,
Uhuru iliyokuwa, yake inayaamua,
Sera za Watanzania, hakuna sera ya chama:
Hasa vya msingi vikiwa !
Wednesday, November 14, 2012
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment