TEKNOHAMA neema, wengi wasioijua,
Nyuma wanaangalia, wanashindwa kusogea,
Hofu imewaingia, kuenea teknolojia,
Tumeshaondoka GB, sasa tunakwenda PB !
Ni ujinga au ujuha, mimi siwezi kujua,
Ni sanaa imekuwa, ukuu bila kujua,
Na tunakoelekea, itageuzwa hadaa,
Tumeshaondoka GB, sasa tunakwenda PB !
Chini tumeng'ang'ania, hatutaki kwenda paa,
Anga zimefunguliwa, mitoni tunaogea?
Twashikilia dagaa, papa tunawaachia?
Tumeshaondoka GB, sasa tunakwenda PB !
Vijana kutoandaa, dhuluma ninahofia,
Mengi yangelitufaa, tungeanza wachochea,
Kuunda wakaingia, yale tusiyodhania,
Tumeshaondoka GB, sasa tunakwenda PB !
Laiti ningelikuwa, jopo ningejiundia,
Kwenye kila tasnia, malengo kujiwekea,
Jinsi ya kuitumia, itufae teknolojia,
Tumeshaondoka GB, sasa tunakwenda PB !
Ila wapo wenye njaa, yao wanajifanyia,
Na uadui kuuzua, udugu unapotakiwa,
Wao wamedhamiria, ndio wa kwanza wakawa,
Tumeshaondoka GB, sasa tunakwenda PB !
Tovuti twaiambaa, kando kando kpitia,
Naweza kukuhesabia, wizara zinazojua,
Nyingi sana zafubaa, si kushoto si kulia,
Tumeshaondoka GB, sasa tunakwenda PB !
Matokeo nasikia, uoza wananunua,
Vyenyewe vinavyochaa, pasina ya kutumiwa,
Yakishapita masaa, vipuli hutoopoa,
Tumeshaondoka GB, sasa tunakwenda PB !
Watani nawatania, japo kikongwe najua,
Njia zangu zimejaa, najua pakupitia,
Dunia kujionea, mengine kuwa mzaha,
Tumeshaondoka GB, sasa tunakwenda PB !
Gigabaiti napaa, terra daraja likawa,
Na sasa ninaingia, picabaiti kuvaa,
Inshallah nikijaliwa, nje naenda chukua,
Tumeshaondoka GB, sasa tunakwenda PB !
Inshallah nikijaliwa, nje naenda chukua,
Masomoni nikitua, Asia kusalimia,
Terrabaiti kutwaa, maajabu kujionea,
Tumeshaondoka GB, sasa tunakwenda PB !
Kinyonga tumeshakua, kobe wanatuzidia,
Polepole twatembea, konokono katuoa,
Mme nyuma twafatia, twaenda pasi hatua,
Tumeshaondoka GB, nyie bado mwachelewa ?
Maofisi yatakiwa, kwa fujo kuitimua,
Vijana kuajiriwa, vyuo inaokokotoa,
Maarifa kuenea, nchi tukainyanyua,
Tumeshaondoka GB, nyie bado mwachelewa ?
Majeshi yanatakiwa, vitengo kuvifungua,
Vitu tukavigundua, hata eropleni pia,
Tweze jiendeshea, ofisini tumekaa,
Tumeshaondoka GB, nyie bado mwachelewa ?
Shuleni inatakiwa, kwa wingi iwe yajaa,
Kama bilauri kuwa, hata chini yajimwaiya,
Ustadi ukakua, vyuoni wakiingia,
Tumeshaondoka GB, nyie bado mwachelewa ?
Vijijini yatakiwa, kawi tukifyatua,
Jua inayotumia, au taka nazo pia,
Rahisi sana ikawa, na gharama kupungua,
Tumeshaondoka GB, nyie bado mwachelewa ?
Viongozi watakiwa, tena sana kuijua,
Vihiyo ninaojua, wa kompyuta wakiwa,
Dhamana waliopewa, na bado waikimbia,
Tumeshaondoka GB, nyie bado mwachelewa ?
Kisha nitanukia, Petabaiti kwingia,
Kichochoro nakijua, eksabaiti kutua,
Kisha nikasalimia, zetabaiti jamaa,
Tumeshaondoka GB, sasa tunakwenda PB !
Zetabaiti najua, siwezi kuifikia,
Naona itachelewa, Yotabaiti kungojea,
Kisha brontobaiti, wajukuu kumjua,
Tumeshaondoka GB, sasa tunakwenda PB !
Taifa la kusinzia, kazi huko kufikia,
Mdebwedo watembea, na usiku waingia,
Uso tukija kunawa, mchana imeshakuwa,
Inshallah nikijaliwa, nje naenda chukua,
Tumeshaondoka GB, sasa tunakwenda PB !
Thursday, November 8, 2012
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment