Friday, November 2, 2012

Kazi ndio imeanza




Kazi ndio imeanza, kujenga demokrasia,

Katiba twatengeneza, ubosi kuuchukua,

Rais tukiamua, pasiwe wa kuzuia,

Mbegu ninawaachia, kupanda mnatakiwa !



Hayawezi wapendeza, utamuni walokaa,

Ajinzi wataifanza, nyufa zipate bakia,

Ili yao kuyatunza, na vya watu kuvitwaa,

Mbegu ninawaachia, kupanda mnatakiwa !



Katiba bila mwangaza, ovyoovyo itakua,

Madudu ikayatunza, watu yasiyosadia,

Hivyo jambo la kufanza, kwanza ni kuielewa,

Mbegu ninawaachia, kupanda mnatakiwa !



Kwanza ni kuyawaza, yakufaa, yasofaa,

Kisha tukabayabwagiza, udhia yanayotia,

Na safi tukayatunza, kizazi kuja kifaa,

Mbegu ninawaachia, kupanda mnatakiwa !



Moja la kuliangaza, rais safi akawa,

Kila kitu kutengeza, na waovu kuwatoa,

Nchi hii kuongoza, raia wanayeridhia,

Mbegu ninawaachia, kupanda mnatakiwa !



Fedha wanaosambaza, mapema kuwagundua,

Na wao kuwabamiza, mbali kutokufikia,

Nchi mwenye kuiweza, fedha kutoabudia,

Mbegu ninawaachia, kupanda mnatakiwa !



Ardhi kutoiuza, jengine kuangalia,

Watu wasije chuuzwa, masikini kubakia,

Hili ninalihimiza, kiranja kusimamia,

Mbegu ninawaachia, kupanda mnatakiwa !



Kulipiga vita giza, hima ninaitoa,

Hatuwezi kuongoza, gizani huku twakaa,

Mwangaza kuueneza, vijijini kusambaa,

Mbegu ninawaachia, kupanda mnatakiwa !



Maji uhai wa kwanza, hili linatangulia,

Kuleta asiyeweza, kitini kumuondoa,

Ifanzike miujiza, yatiririke Tanzania,

Mbegu ninawaachia, kupanda mnatakiwa !



Afya watu kutokwaza, budi bure kutoa,

Kile tunachoingiza, migodini kutumiwa,

Hili kwenu naagiza, sera ninawaachia,

Mbegu ninawaachia, kupanda mnatakiwa !



Elimu nayo kutunza, muhimu bure kutoa,

Kusawazisha yaweza, umma wote Tanzania,

Na kila anayeweza, fedha kikwazo kutokuwa,

Mbegu ninawaachia, kupanda mnatakiwa !



Maliasili kutunza, vizazi ikawafaa,

Na vyanzo kuendeleza, uhai kutochezewa,

Maisha kutochuuza, mengine ni kukataa,

Mbegu ninawaachia, kupanda mnatakiwa !

No comments: