Sunday, November 18, 2012
Mwizi wa fikira
Mwizi wa fikira mwizi, kingine hawezi kuwa,
Tabiaye udokozi, ya watu kuyachukua,
Kisha kwenda kuyahodhi, kuwa yake kujitia,
Fikra mwenye kuiba, sikuzote huwa mwizi !
Watazame waenezi, jinsi wanavyodokoa,
Hii ndiyo yao kazi, sasa wanaajiriwa,
Na utundu hawawezi, jema wakalipanua,
Fikra mwenye kuiba, sikuzote huwa mwizi !
Wageuka wachuuzi, wakubwa kuwauzia,
Wakaachia machozi, Baadi kuwaachia,
Mrahaba kuwaizi, ya kwao wakajilia,
Fikra mwenye kuiba, sikuzote huwa mwizi !
Anayaona mwenyezi, sadaka sasa watoa,
Kwake bado wana enzi, siku ya kuahidiwa,
Kisha wote majambazi, huko kwenda kudaiwa,
Fikra mwenye kuiba, sikuzote huwa mwizi !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment